Mwenyekiti wa Kikundi cha Waendesha pikipiki Likotwa Manispaa ya Lindi, Bw. Maulid Said Mohamed (kushoto) akimkabidhi Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Vijana, Bw. James Kajugusi  risala kuhusu kikundi hicho  hivi karibuni  Mjini Lindi. Mkurugenzi huyo alitembelea kikundi hicho ili kukagua jinsi kikundi hicho kinavyofanya kazi na jinsi kinavyonufaika na umoja huo. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi Manispaa ya Lindi, Bw. Daniel Kanuse.(Picha na: Concilia Niyibitanga).
======== ======= =======
Serikali kukopesha vikundi 453 vya Vijana

Na: Concilia Niyibitanga - Afisa Habari Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo

Serikali inatarajia kukopesha vikundi vya uzalishaji mali vya vijana vipatavyo 453 katika mwaka wa fedha 2014/15 kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana. Hayo yamesemwa hivi karibuni na Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Vijana, Bw. James Kajugusi alipotembelea kikundi cha Vijana waendesha pikipiki cha Likotwa kilichopo Halmashauri ya Manispaa ya Lindi.

Lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa vijana wanajiajiri wenyewe na kuondokana na dhana ya kutegemea kuajiriwa ikizingatiwa kuwa kila mwaka vijana wapatao milioni 1.2 huhitimu vyuo vikuu lakini wanaopata ajira za kuajiriwa ni vijana 200 tu. Amesema Bw. Kajugusi.

Mikopo inayotolewa kwa vijana kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ni njia ya kuwakomboa vijana kwa kuwaongezea mitaji ya kuweza kufanya shughuli za ujasiri na ujasiriamali na hatimaye kujiajiri na kuajiri vijana wenzao.

Bw. Kajugusi amekipongeza Kikundi cha Waendesha pikipiki maarufu kama bodaboda cha Likotwa kwa juhudi na mafanikio waliofikia hadi sasa kutokana na kuunda kikundi hicho chenye lengo la kuboresha maisha ya waendesha pikipiki hao.Aidha, amewataka kuzingatia  sheria za usalama  barabarani, kuzingatia maadili mema ili kuimarisha amani  na mshikamao katika sehemu wanazoishi na vile vile  kuhakikisha wanatimiza wajibu wao kama vijana wa kulipa kodi.

Halikadhalika, amekitaka kikundi hicho kuwahamasisha vijana wenzao kushiriki katika shughuli za Mbio za Mwenge wa Uhuru na kuwaeleza manufaa ya mbio hizo na kuwapuuza wanobeza Mwenge kwani wanaoubeza ni watumwa kwani  wanaibeza historia ya nchi yao.

Naye kwa upande wake Mwenyekiti wa Kikundi hicho, Bw. Maulid Said Mohamed  amesema kuwa kikundi kina wanachama 13 na pikipiki 2 zinazomilikiwa na kikundi  na hadi sasa wameshapatiwa viwanja 6 na Uongozi wa Manispaa kwa ajili ya kufanya shughuli za maendeleo ya Kikundi.

Bw. Mohamed amesema kuwa mpaka sasa kikundi kimejiwekea akiba na lengo kuu ni kuanzisha SACCOS kwa ajili ya kuwakopesha vijana kwa riba nafuu na hatimaye kutengeneza ajira kwa vijana wengi zaidi.

Kikundi cha Waendesha pikipiki Likotwa kina wanachama 13 na kilianzishwa kwa nia ya kusaidiana na kujiinua kiuchumi na kina malengo ya kuanzisha SACCOS kwa ajili ya kukopesha vijana mikopo yenye masharti nafuu.
MWISHO 


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...