Mkurugenzi Sera na Utafiti wa TRA Bw. Tonedeus Muganyizi akizungumza
na wana umoja wa uingizaji na uuzaji wa kazi za filamu na muziki zinazotoka nchi za
nje wakati wa kikao cha wafanyabiashara hao na asasi zinazosimamia usambazaji na
uuzaji wa kazi za filamu na muziki jana jijini Dar es Salaam.
Wadau mbalimbali wakijadiliana wakati wa kikao cha wafanyabiashara na
asasi zinazosimamia usambazaji na uuzaji wa kazi za filamu na muziki jana jijini Dar
es Salaam.
Na Genofeva Matemu – Afisa Mawasiliano Serikalini WHVUM
Mkurugenzi Sera na Utafiti kutoka TRA Bw. Tonedeus Muganyizi amevitaka vyombo
vya udhibiti vya kiserikali kufanya kazi kwa pamoja na TRA katika kusimamia sheria na
kanuni za usambazaji na uuzaji wa kazi za Filamu na muziki nchini.
Rai hiyo jana jijini Dar es Salaam wakati wa kikao kilichowahusisha wafanyabiashara
wanaosambaza kazi za filamu na muziki pamoja na wadau wanaohusika na usimamizi
wa usambazaji wa kazi za filamu na muziki kutoka TRA, Bodi ya Filamu, BASATA,
pamoja na COSOTA baada ya wafanyabiashara hao kuwasilisha maombi yao kuhusiana
na operesheni inayoendelea ya kukamata kazi za filamu na muziki zinazotoka nje ya
nchi zisizokuwa na haki miliki na stempu ya TRA.
Aidha Bw. Muganyizi amesema kuwa kazi yoyote ya filamu na muziki inapaswa kuwa
na haki miliki kabla ya kusambazwa ili kuiwezesha TRA kutoa stempu kwa kazi hizo
jambo ambalo limekuwa likikiukwa na wafanyabiashara wanaosambaza na kuuza kazi
hizo hivyo kupelekea Serikali kuendesha operesheni ya kusaka kazi za filamu na muziki
zisisokuwa na haki miliki na stempu kutoka TRA.
Akitoa mchango wake Katibu Mtendaji kutoka Bodi ya Filamu Bibi. Joyce Fisoo
amewataka wafanyabiashara wa kusambaza na kuuza kazi za filamu na muziki
zinazotoka nje ya nchi na za hapa nchini kufuata sheria na kanuni zilizowekwa ili
kuweza kulinda mali zao na kufanya biashara kwa amani.
Bibi. Fisoo amesema kuwa kifungu cha 19, 1 cha sheria ya haki miliki ya mwaka 1996
kimefafanua kuwa uuzaji, usambazaji, ukodishaji na uonyeshaji wa filamu za picha
jongevu uzingatie usajili kutoka Bodi ya Filamu kuziwezesha kazi hizo kuwa halali
zinaposambazwa.
Naye Afisa Mtendaji Mkuu kutoka COSOTA Bibi. Doris Antony amewataka
wafanyabiashara kuheshimu haki miliki za wasanii kwani mmiliki wa kazi ya filamu
na muziki ana haki 9 ambapo kati ya haki hizo tisa ni pamoja na haki ya kusambaza
kazi yake, haki ya kuzalisha, haki ya kutafsiri, haki ya kuonyesha kwa Umma, haki ya
kupeleka kwenye vyombo vya habari pamoja na haki ya kupeleka nje ya nchi.
Wakitoa mchango wao, wanaumoja wa uingizaji na uuzaji wa kazi za filamu na muziki
zinazotoka nje ya nchi wameiomba serikali kuwapa nafasi kumalizia mzigo uliopo
sokoni kwa madai kuwa hawakuwa na ufahamu wa sheria inayosimamia haki miliki kitu
ambacho serikali imekipinga na kuwataka kufuatilia haki miliki ya kazi walizonazo kwa
wamiliki kuiwezesha serikali kutoa stempu zitakazowawezesha kuuza kazi hizo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...