Walimu
na wanafunzi wa shule ya sekondari Iwawa iliyopo Makete mkoani Njombe
wametakiwa kutoridhika na kubweteka na shule hiyo kushika nafasi ya nne
kitaifa katika matokeo ya kidato cha sita 2014 yaliyotangazwa miezi
michache iliyopita
Kauli
hiyo imetolewa na mkuu wa wilaya ya Makete Mh. Josephine Matiro katika
hafla ya kuwapongeza walimu wa Iwawa sekondari baada ya shule hiyo
kushika nafasi ya 4 kitaifa, nafasi ya 2 kikanda na nafasi ya 1 kwa mkoa
wa Njombe katika matokeo ya kidato cha sita mwaka huu
Amewapongeza
walimu kwa jitihada zao za kufundisha pamoja na moyo wa wanafunzi
katika kujisomea ambavyo kwa pamoja vimepelekea kuitangaza wilaya ya
Makete kielimu na kuwataka kupanda na kushika nafasi za juu katika
mitihani inayofuata
"Ni
kweli mnastahili pongezi lakini nawaombeni ongezeni bidii ili mitihani
inayokuja mwakani mpande zaidi ya hapa, muitangaze wilaya yetu,
tukishirikina pamoja tunaweza" amesema Matiro
Katika
hatua nyingine mkuu huyo wa wilaya amewataka wananchi kushirikiana
katika kuchangia maendeleo ya shule kwani serikali inaunga mkono
jitihada zao pale tu inapoona wamechangia
Amesema
kumekuwa na kasumba ya watu wachache kuwakatisha tamaa wananchi wengi
wenye moyo wakuchangia miradi ya shule, na kusema wananchi wasikatishwe
tamaa na watu wa aina hiyo kwani serikali haiwaachii peke yao, wao
wakichangia kwa kiasi fulani serikali nayo humalizia palipobakia huku
akisisitiza kuwa kwa shule zenye upungufu wa walimu, serikali
inalitambua tatizo hilo na ndiyo maana inapanga walimu wapya kila mwaka
katika shule hizo na mwishowe upungufu huo utamalizika
Awali
akisoma taarifa ya shule kwa mkuu wa wilaya, mkuu wa shule hiyo Mwl.
Antony Ng'wavi amesema shule yake inakabiliwa na changamoto mbalimbali
ikiwemo upungufu wa vyumba vya madarasa pamoja na walimu jambo ambalo
linachangia kupungua kasi ya ufaulu kwa kiasi kikubwa zaidi, huku
akiahidi kuwa mwakani shule yake itafanya vizuri kuliko mwaka huu
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...