.jpg)
Mkurugenzi wa Mambo ya Kale katika Wizara ya Maliasili na Utalii, Bw. Donatius M.K. Kamamba (pichani) ametunukiwa tuzo ya kimataifa ya “The knight Cross in the Order of Arts and Letters” na Serikali ya Ufaransa.
Hatua hiyo imetokana na mchango mkubwa alioutoa Bw. Kamamba katika kulinda na kuendeleza Urithi wa Utamaduni hapa nchini na duniani kwa ujumla katika kipindi cha miaka 33 aliyoitumikia sekta ya malikale ndani na nje ya nchi.
Katika barua aliyoandikiwa Mkurugenzi huyo na Balozi wa Ufaransa hapa nchini, Balozi Marcel Escure, amesema kuwa Bw. Kamamba amekuwa mstari wa mbele katika kusimamia na kuendeleza rasilimali za malikale na kuimarisha mahusiano kati ya Tanzania na Jumuia ya Kimataifa.
Bw. Kamamba atatunukiwa tuzo hiyo na Balozi Escure katika Ubalozi wa Ufaransa uliopo nchini Septemba 3, 2014 saa sita mchana.
Tuzo hiyo ilianzishwa mwaka 1957 kwa kutambua mchango wa wasanii maarufu na waandishi waliochangia kwa kiasi kikubwa kuendeleza sanaa nchini Ufaransa na duniani kote.
Tuzo ya “The knight Cross in the Order of Arts and Letters” hutolewa nje ya Ufaransa mara tatu kila mwaka chini ya Mamlaka ya Waziri wa Utamaduni na Mawasiliano ya Umma.
Ametunikiwa sawa, lakini tujaribu kuangalia hali ya uhifadhi wa malikale zetu hapa nchini. Hongera sana, ushauri boresha malikale za nchi yetu.
ReplyDelete