Na Bashir Yakub
Hapo  awali  niliandika  namna  sheria isivyowaruhusu  viongozi  wa  serikali  za mitaa  kuandaaa  na  kusimamia  mauzo  na manunuzi  ya nyumba au viwanja. Nikasema  kitu hicho  hakiruhusiwi  katika  sheria  na wanaofanya  hivyo  hakika  wako  katika  makosa  makubwa.  Nikasisitiza kuwa  wewe ambaye  mkataba  wako  umeandikiwa serikali za mitaa  ujue wazi  kuwa mkataba wako wa manunuzi   hauna  hadhi  kisheria. Huu ni ukweli  ambao  nitazidi  kuusema ili  kuwaepusha watu  na usumbufu  na ili watu  wasiendelee  kuingia  katika  utapeli  huu. Ndio,  huu ni utapeli  na ni jinai.   Ni  sababu  hizihizi  zinazowaingiza watu  wasio  na hatia kwenye  migogoro ya ardhi  na kuwapotezea  hela  zao.

1.HUWEZI  KUFANYA  TRANSFER  UKIWA  NA MKATABA  WA SERIKALI  ZA  MITAA.
Kwa wale  ambao  waliwahi  kufanyia  mikataba  yao  ya manunuzi  ya nyumba/viwanja  serikali  za mitaa halafu  wakaamua  kwenda ardhi  kubadili  jina  watakuwa wamekutana  na  hiki  kitu  ninachoongelea hapa.  Ikiwa ulifanya manunuzi  ya ardhi na  ukasimamiwa  na serikali za mitaa basi  ujue  huwezi kubadilisha  jina  kutoka  kwa  aliyekuuzia  kuingia  jina  lako. Na  hapo  ni  vyote  yaani  hati  au leseni  ya makazi. Huwezi  kabisa kubadilsha  kimojawapo  kati  ya hivyo  ikiwa  mkataba wako ni wa serikali  za mitaa.

2.KWANINI  UTAKATALIWA  KUBADILI  JINA.
Sababu  ni ilieile   kuwa  mkataba  wa serikali  za mitaa  si  mkataba  rasmi wa kisheria.  Ni  mkataba  kama mikataba    ya  mitaani ambayo  mtu anaweza kuchomoa  karatasi  kwenye  daftari dogo  la  mwanae  la shule  halafu mkaandikiana.  Hauna  hadhi ya  kisheria  ndio maana  mamlaka  za ardhi  hazikubali  uutumie  kubadilisha  jina. Ifikie  hatua  watu  wayaelewe kwa dhati  haya.

3. HUWEZI  PIA  KUUTUMIA  KUTAFUTIA  HATI/LESENI  YA  MAKAZI.
Hapo juu  nimezungumzia  kufanya  transfer  kwa  wanao nunua sehemu ambazo tayari  zina hati, ofa   au  leseni  za  makazi.  Lakini kuna maeneo  ambayo  hayana  hati, ofa  wala leseni za makazi. Haya  ni maeneo  ambayo  mtu  akinunua  huanza  na  moja  kutafuta  vitu  hivi.  Basi ikiwa  mtu  amefanya  mkataba  serikali  za mitaa halafu  anataka  kuanza  na  moja  kutafuta vitu hivi   ajue  wazi kuwa   mkataba  huo  kamwe  hauwezi  kukusaidia  kupata  hati  wala  leseni ya  makazi.  Ukienda  mamlaka  za ardhi  na mkataba  wako huo  hakuna  shaka  yoyote  isipokuwa  lazima  ukataliwe  tu.  Kwa asiyeamini  basi  na ajaribu.

4.NINI  UFANYE  IKIWA  TAYARI UNA  MKATABA  WA SERIKALI  ZA MITAA  NA  UNATAKA  KUBADILI  JINA  AU  KUPATA  HATI.
Ili ukubaliwe  kufanya  transfer au  kupata  hati  iwapo una  mkataba  wa serikali  za mitaa  basi  huna budi kuandikiwa mkataba  mpya  na mwanasheria  ambao  pia  ataudhibitisha  kwa muhuri  maalum. Nje ya hatua  hii  huwezi  kupata  hati  wala  kufanya  transfer . Hili  ni jambo ambalo  halikwepeki  na ndio  maana  huwa  tunapenda  kuwasisitiza  watu  kufanyia  mikataba  yao  kwa wanasheria     kuepuka  usumbufu  badae.

5. UTAFANYAJE  MKATABA  MPYA  WA KISHERIA  IWAPO  ALIYEKUUZIA  AMEKUFA  AU HUJUI  ALIPO.
Inawezekana  wakati  wa kununua  ulifanya  mkataba  serikali za mitaa  na sasa unataka  kupata  hati  au  kubadili  jina  lakini  aliyekuuzia amekufa  au hujui pakumpata  ili ufanye naye  mkataba mpya  wa kukuwezesha  kupata vitu hivyo.   Au umepata taarifa  za makala  haya  na  sasa  unataka  kufanya  mkataba  mpya  wa kisheria  lakini  hapohapo  hujui aliyekuuzia alipo   au una taarifa amekufa.  Jibu  la sintofahamu hii ni kuwa upo  utaratibu  maalum  wa kisheria  wa kurahisisha  jambo hili. Kwanza  upo utaratibu  wa kimirathi  lakini  pili  upo  utaratibu  wa Next  of Kin  na  kiapo.  Utaratibu  huu utakuwezesha  kuandika  mkataba  mpya  unaokubalika  katika  kufanya  transfer  au  kupata  hati  bila  kuwepo  aliyekuuzia.

6. USHAURI   WA   KITAALAM.
Usipende  kufanya  mambo  kienyeji  katika  masuala  ya  msingi  sana  kama ardhi. Ikiwa unataka  kununua ardhi  hata   kama  ni ndogo  kiasi  gani  mtafute  mwanasheria  yeyote  akusimamie  mkataba  wako  ili  uepuke  usumbufu  wa baadae. Hi ni kwasababu hali  ilivyo  hata  ukisema  simtafuti  mwanasheria  itakuwa  ni kazi  bure  kwakuwa  mwisho  wa siku ni lazima utamtafuta  tu  la  sivyo ukubali  kukaa  na ardhi  ambayo  haina  hati  au  ambayo  ina  hati/leseni  ya makazi lakini milele  ikae  kwenye  jina  la  aliyekuuzia.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.     0784482959, 0714047241

bashiryakub@ymail.com

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...