Na Ally Rashid Dilunga, London
Katika kukamilisha mojawapo ya malengo ya ziara yake ya kikazi hapa Uingereza, Naibu waziri wa viwanda na biashara Mheshimiwa Janet mbene, amemalizia ziara yake ya wiki moja nchini Uingereza kwa kukutanishwa na baadhi ya wafanyabiashara wa Kitanzania hapa Ubalozini jijini London.
Ametumia fursa hiyo kuwafahamisha hatua zinazochukuliwa na Serikali kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji na pia kuwataarifu juu ya fursa za kibiashara zilizoko katika sekta mbalimbali nchini Tanzania na kuwahamasisha kuzichangamkia fursa hizo na wasiwe ni wenye kuwaachia tu wanufaike nazo wageni.
Amewaambia kuwa kuna njia nyingi za kujishughulisha kibiashara, kuanzia kwao wenyewe kuwa ni sehemu ya masoko kwa kuwa waagizaji na wasambazaji wa bidhaa za Kitanzania, au kwa kushawishi wawekezaji kuja kuwekeza katika miradi mbalimbali nchini au kuingia nao ubia.
Hata hivyo nao walimlalamikia Mheshimiwa Naibu Waziri juu ya ukosefu wa taarifa za biashara juu ya miradi ya uwekezaji nchini, ambapo naye amekiri upungufu huo na kwamba ushauri wao ameuzingatia.
Tangu alipowasili nchini Uingereza, Mheshimiwa Mbene alikutanishwa na wafanyabiashara na wawekezaji mbalimbali kupitia Vyama vyao vya kibiashara na pia alikutana na baadhi ya wafanyabiashara na wawekezaji binafsi na kufanya nao mazungumzo yenye lengo la kuwekeza kwenye uongezaji thamani wa mazao au kufanya biashara hasa kwa kuvipatia masoko bidhaa kutoka nchini Tanzania.
Viongozi wa vyama vya kibiashara na baadhi ya wanachama wao aliokutanishwa nao ni wa Eastern Africa Association (EAA), Business Council for Africa (BCA) na UK-Tanzania Business Group.
Mheshimiwa Janet Mbene pia alikutanishwa na mshauri wa Serikali ya Uingereza juu ya masuala ya biashara kwa Tanzania, Lord Clive Hollick na watendaji wengine wa Idara ya uhamasishaji uwekezaji na Biashara (UKTI), ambapo alielezwa baadhi ya changamoto wanazokumbana nazo wawekezaji nchini Tanzania. Mheshimiwa Mbene alitumia fursa hiyo kuwapa ushauri anaoamini utasaidia kupatikana kwa ufumbuzi wa changamoto hizo na hasa baada ya mifumo ya utendaji kazi serikalini kurekebishwa kupitia Mpango maalum wa Matokeo Makubwa sasa (BRN).
Katika siku ya tatu ya ziara yake, mheshimiwa Mbene alitembelea Ofisi za Ubalozi na kukutana na watumishi wa Ubalozi na baadaye kukitembelea Kituo cha Biashara na kupata maelezo juu ya shughuli zake na changamoto zake.
Pia kutokana na ziara yake na kuongea na wafanyabiashara mbalimbali, Mheshimiwa Mbene amegundua kuwa Kituo kinafanya kazi kwa karibu sana na wafanyabiashara wa Ulaya, hivyo Serikali inatakiwa kukiongezea Kituo nguvu zaidi ili kiweze kutekeleza majukumu yake mengi kwa ufanisi zaidi na kuendelea kutoa mchango wake mkubwa katika kufanikisha malengo ya kiuchumi ya Taifa, kama ilivyokusudiwa.
Mheshimiwa Mbene baada ya kugundua kuwa ziko fursa nyingi za biashara na uwekezaji na kwamba wafanyabiashara wengi wana imani na Tanzania, ameahidi kupeleka mapendekezo yake Serikalini ya jinsi ya kuimarisha shughuli za Vituo vyetu vya Biashara ambavyo viko nje ya Tanzania.

 Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Tanzania, Mheshimiwa Janeth Mbene(kulia), akiongea na Mwakilishi wa Serikali ya Uingereza katika masuala ya Biashara na Uwekezaji nchini Tanzania, Lord Clive Hollick, walipokutana kuzungumzia masuala ya Biashara ya kati ya nchi mbili ya Tanzania na Uingereza na juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Uingereza kusaidia wawekezaji wa Kiingereza kuwekeza Tanzania.
 Mheshimiwa Janeth Mbene, akiongeza na Wawekezaji na Wafanyabiashara wa Kiingereza alipokutana nao kwa mwaliko wa Kituo cha Biashara cha Tanzania, London na Jumuiya ya Wafanyabiashara wa East African Association. Mheshimiwa Naibu Waziri alikutana na Wafanyabiashara hao kwa lengo la kuwashawishi kuja kuwekeza nchini Tanzania
 Mheshimiwa Waziri Janeth Mbene(kulia), alipokutana na Mwakilishi wa Serikali ya Uingereza na Chama cha Wafanyabiashara na Wawekezaji wa nchini Uingereza (UKTI) (kati mwa picha), kushoto ni Mkurugenzi wa Kituo cha Biashara cha Tanzania nchini Uingereza, Bwana Yusuf Kashangwa.
 Wawakilishi wa Jumuiya za Wafanyabiashara na Wanachama wa chama cha Wafanyabiashara wa Tanzania nchini Uingereza (Tanzania Business Group) wakimsikiliza Naibu Waziri wa Viwanda, Mheshimiwa Janeth Mbene, alipokutana na kuzungumza nao siku ya Ijumaa tarehe 28 Februari 2015, mkutano uliofanyika katika Ukumbi wa Ofisi za Ubalozi wa Tanzania, London. Mheshimiwa Waziri alikutana nao kuzungumzia hali ya Siasa na Uchumi na maendeleo ya nchi kwa ujumla. Mheshimiwa Waziri aliwakumbusha Wafanyabiashara hao kutumia fursa zilizopo na kuwekeza nyumbani Tanzania, kwa lengo la kuongeza ajira na kuinua uchumi wa nchi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...