Waziri wa Ujenzi Dkt.
John Magufuli ametangaza kutobomolewa nyumba zilizopo kando kando ya barabara ya Mwanga-Kikweni/Vuchama-hadi Lomwe
km 40.6 na kusema kuwa barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami kwa kutumia
upana wake uliopo hivi sasa.
Dkt. Magufuli alitoa
kauli hiyo ya faraja kwa wakazi wa Kikweni Wilayani Mwanga Mkoani Kilimanjaro
kabla ya kuweka jiwe la msingi katika barabara ya Mwanga-Kikweni/Vuchama-Usangi
hadi Lomwe(km 40) itakayojengwa kwa kiwango cha lami hivi karibuni.
Waziri wa Ujenzi
amechukua uamuzi huo kutokana na maeneo mengi ya milimani ambapo barabara hiyo inapita
kuwa na mashamba ya watu tofauti na sehemu nyingine.
“Nikiwa kama Waziri wa
ujenzi katika maeneo haya ya milima sitatumia sheria ya mita 30 kila upande
katika ujenzi wa barabara hii ili nyumba na mashamba ya wakazi wa huku
yasiathirike”
Dkt. Magufuli
aliongeza kuwa ujenzi wa Barabara una sheria zake ndio maana ameamua kutumia
sheria ya barabara namba 13 ya mwaka
2007 kifungu cha 13 na 20 kinachompa mamlaka kupunguza upana wa barabara
Aidha, Waziri Magufuli
aliwatoa hofu wakazi wote waliowekewa alama ya X katika nyumba zao na kuwataka
kuendelea na shughuli zao kama kawaida kwasababu nyumba hizo hazitabomolewa.
Katika hatua nyingine
Dkt. Magufuli aliwataka watu wote waliojenga vibanda karibu na barabara ya
zamani waanze kuondoka mapema kabla ya ujenzi wa barabara hiyo kuanza hivi
karibuni.
“Nawaomba wote
mlioweka vibanda karibu na barabara mtoe kwa hiari yenu ili tutengeneze
barabara hii bila vikwazo na kwa haraka tofauti na awali ambapo tulikuwa
tunatangaza zabuni kwa kilomita chache” alisisitiza Waziri Magufuli
Kwa upande wa Mkuu wa
Mkoa wa Kilimanjaro Leonidas Gama amemshukuru Waziri Magufuli kwa hatua yake
hiyo na kusema kuwa kufunguka kwa barabara hiyo ni mkombozi mkubwa kwa wilaya
ya Mwanga na Mkoa wa Kilimanjaro kwa ujumla.
“Wilaya yetu hii
inapakana na nchi jirani hivyo hata kiusalama ni vizuri barabara hii ikajengwa
kwa lami ili irahisishe mawasiliano kwa haraka zaidi katika Wilaya yetu hii”
alisema Mkuu wa Mkoa
Naye Mbunge wa Mwanga
ambaye pia ni Waziri wa Maji Profesa Jumanne Maghembe ameishukuru Serikali na
kusema kuwa kukamilika kwa barabara hiyo kutawaondolea kero kubwa ya usafiri
wananchi wa Usangi na mwanga na kuwasaidia kufanya biashara kwa urahisi zaidi
tofauti na awali.
“Kukamilika kwa
barabara hii kutasaidia kuinua uchumi mkubwa uliopo huku Usangi tofauti na hali
iliyopo sasa” Alisema Profesa Maghembe.
Waziri wa Ujenzi Dkt. John Pombe Magufuli katikati akiweka jiwe na msingi kuashiria kuanza kwa ujenzi wa barabara ya Mwanga-Kikweni-Vuchama-Usangi-Lomwe yenye urefu wa kilomita 40. Kulia kwake ni Waziri wa Maji ambaye pia ni Mbunge wa Mwanga Profesa Jumanne Maghembe, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Leonidas Gama pamoja na viongozi wengine wa Wilaya ya Mwanga.
Waziri wa Ujenzi Dkt. John Pombe Magufuli kushoto akizungumza jambo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi Eng. Musa Iyombe kabla ya kuweka jiwe la msingi katika barabara ya Mwanga-Kikweni-Vuchama-Usangi-Lomwe yenye urefu wa kilomita 40.6. Katikati ni Waziri wa Maji ambaye pia ni Mbunge wa Mwanga Profesa Jumanne Maghembe.
Waziri wa Ujenzi Dkt. John Pombe Magufuli akiwa pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Leonidas Gama wakicheza ngoma na kikundi cha ngoma za asili Kikweni kabla ya uzinduzi wa barabara ya Mwanga-Kikweni-Vuchama-Usangi-Lomwe yenye urefu wa kilomita 40.
. Waziri wa Ujenzi Dkt. John Pombe Magufuli akipiga ngoma na kikundi cha ngoma cha Msanja group kabla ya kuhutubia mamia ya wakazi wa Usangi kuhusu ujenzi wa barabara ya Kikweni-Usangi-Lomwe ambayo itaanza kujengwa hivi karibuni.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...