Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Sadick,
ameitaka Bohari ya Dawa MSD kuendeleza
kasi ya huduma zake za kupambana na ugonjwa wa malaria kwakuwa ni moja ya taasisi zilizo mstari wa mbele kupunguza vifo
vitokanavyo na ugonjwa huo.
Akizungumza jana katika banda la MSD ikiwa ni
maadhimisho ya siku ya Malaria duniani Sadick alisema MSD imekuwa ikifanya
jitihada kuhakikisha ugonjwa wa malaria unakoma na vifo vitokanavyo na ugonjwa
huo vinapungua.
Alisema jitihada hizo za MSD zimechangia
matokeo ya kupungua takwimu za vifo vya mama na mtoto mchanga chini ya miaka
mitano vitokanavyo na ugonjwa wa malaria hivyo jitihada zaidi zinahitajika
kuhakikisha malengo ya millennia ya kupunguza vifo hivyo yanafikiwa.
Alisema kutokana na MSD kuhakikisha dawa za
malaria zinapatikana katika kila kituo cha afya, Zahanati na Hospitali ni
wajibu wa wananchi kuhakikisha wanafanya
matumizi sahihi ya dawa hizo ili kutibu ugonjwa huo.
“MSD inasaidia serikali kufikia lengo la
kupunguza ugonjwa wa malaria tumeelezwa jinsi gani MSD inahakikisha dawa za
malaria hazikosekani katika vituo vya kutolea huduma lakini pia imepanua wigo kwa kutoa elimu kwa vitendo jinsi ya
kupambana na ugonjwa huo kwa kuhakikisha
kinga dhidi ya malaria inaanzia kwa wafanyakazi wake na wanapewa
vyandarua vyenye dawa wao na familia zao,”alisema
Sadick aliwataka wananchi kuacha kutumia dawa
hizo katika matumizi yasiyo sahihi ikiwemo dozi moja ya dawa kutumiwa na watu
zaidi ya mmoja kwakuwa kufanya hivyo kunasababisha matibabu ya wagonjwa wa
malaria kutokukamilika na kusababisha vifo.
Alisema pia kumekuwepo na matumizi yasiyo
sahihi katika vyandarua vya msaada
ambapo utumika kwa ajili ya kufugia Kuku au kuvulia Samaki hivyo mapambano
dhidi ya ugonjwa huo kutokufanikiwa.
“ Jitihada hizi za MSD na wafadhili mbalimbali
katika kuweka nguvu ya kupambana na Malaria ni wajibu wa jamii kuziunga mkono kwakuwa matumizi ya
misaada hiyo ikiwemo Vyandarua ikitumiwa kwa malengo yaliyokusudiwa kutaongeza uzalishaji wa uchumi katika nchi
kutokana na kuimarika kwa afya ya wananchi wake,”alisema.
Katika maadhimisho hayo Mkuu Mkoa huyo alizindua
mpango wa ugawaji wa Vyandarua milioni 24 kwa nchi mzima ikiwa ni jitihada za
Serikali na wadau mbalimbali kupambana na ugonjwa wa Malaria.
Ofisa
wa Kitengo cha Udhibiti Ubora wa MSD, Richard Makalla (kulia),
akimuelekeza jambo Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Sadiki
alipotembelea banda la MSD katika maadhimisho hayo. Kushoto ni Ofisa
Huduma kwa Wateja Kanda ya Dar es Salaam wa MSD, Florida Sianga na ofisa
kutoka ofisi ya mkuu wa mkoa.
Muenekano wa banda la MSD katika maadhimisho hayo.
Ofisa
Huduma kwa Wateja Kanda ya Dar es Salaam wa MSD, Florida Sianga
(kushoto), akimuelekeza jambo kijana aliyetembelea banda la MSD katika
maadhimisho hayo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...