Na Veronica Simba
Wizara ya Nishati na Madini inapanga kushirikiana na Kampuni ya Mitsubishi Hitachi Power System ya Japan katika kuendeleza sekta ya nishati nchini.
Kamishna Msaidizi wa Umeme wa Wizara, Mhandisi Innocent Luoga aliyasema hayo mapema leo baada ya kukutana na uongozi wa juu wa kampuni hiyo, Makao Makuu ya Wizara jijini Dar es Salaam.
Mhandisi Luoga alisema katika kikao hicho, Ujumbe wa kampuni ya Mitsubishi Hitachi Power Systems Ltd uliwasilisha mapendekezo ya matumizi ya teknolojia ya kisasa ya kufua umeme kutokana na vyanzo mbalimbali ikiwemo makaa ya mawe, jotoardhi na gesi.
“Sisi kama Serikali, kupitia taasisi zetu tumeona ni vema tushirikiane na Kampuni hii ambayo inajishughulisha na kutengeneza mitambo ya kufua umeme wa gesi, makaa ya mawe na jotoardhi kwa kutumia teknojia ya kisasa. Hii ni kutokana na vyanzo vipya vya umeme tulivyonavyo hususan makaa ya mawe na jotoardhi, ambavyo hatujaanza rasmi kuvitumia kuzalisha umeme,” alisema Kamishna Luoga.
Aliongeza kuwa, lengo la Serikali ni kuhakikisha umeme wa kutosha, wa uhakika na wa bei nafuu unazalishwa na kusambazwa nchini ili kuwaletea wananchi maendeleo na hivyo kuinua pato la Taifa kwa ujumla.
Alisema kuwa, Kampuni hiyo ilishafanya majadiliano kuhusu ushirikiano katika sekta ya nishati na taasisi zilizo chini ya Wizara ambazo ni Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Kampuni ya Uendelezaji Jotoardhi Tanzania (TGDC) pamoja na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO).
Akizungumzia kuhusu faida za matumizi ya teknolojia hiyo ya kisasa inayotumika kufua umeme, Kamishna Luoga alizitaja kuwa ni pamoja na kuwa rafiki wa mazingira, kuwezesha uhakika wa kufua umeme kwa bei nafuu pamoja na kufua umeme kwa ufanisi mkubwa.
Awali, katika kikao hicho baina ya Wizara na Kampuni hiyo, Rais wa Kampuni, Takato Nishizawa alisema kampuni yake iko tayari kutoa mafunzo ya namna ya kutumia mitambo yao inayotumia teknolojia hiyo ya kisasa kwa Wahandisi wa kitanzania.
Aidha, Nishizawa alitoa mwaliko kwa wataalamu hao kutoka Tanzania, kutembelea mitambo hiyo huko Japan kwa lengo la kujifunza zaidi.
Katika hatua nyingine, ilielezwa kuwa Kampuni ya Mitsubishi Hitachi Power System Ltd, tayari imeingia mkataba na Kampuni ya Sumitomo ambayo inatekeleza Mradi wa Kufua Umeme wa gesi wa Kinyerezi II unaofikia kiasi cha Megawati 240, kwa kazi ya kufunga mitambo ya kufua umeme (gas turbines) aina ya Hitachi.
Wataalamu wa Wizara
ya Nishati na Madini (Kushoto) wakiwa katika Kikao na Wataalamu wa Kampuni ya
Mitsubishi Hitachi Power System Ltd (Kulia). Kikao kilijadili kuhusu
ushirikiano katika sekta ya nishati na kilifanyika Mei 12, 2015 Makao Makuu ya
Wizara, Dar es Salaam.
Rais wa Kampuni ya
Mitsubishi Hitachi Power System Ltd, Takato Nishizawa (Kulia), akitoa ufafanuzi
kuhusu shughuli zinazofanywa na Kampuni yake kwa Wataalamu wa Wizara ya Nishati
na Madini (Kushoto), wakati wa Kikao kilichokutanisha pande hizo mbili Makao
Makuu ya Wizara jijini Dar es Salaam, Mei 12, 2015 kwa lengo la kujadili
ushirikiano katika sekta ya nishati.
Makamu Rais wa
Kampuni ya Mitsubishi Hitachi Power System Ltd, Satoshi Uchida (Kulia),
akifafanua jambo kwa Wataalamu wa Wizara ya Nishati na Madini, wakati wa kikao
baina yao kilichojadili ushirikiano katika sekta ya nishati. Kikao kilifanyika
Mei 12, 2015 Makao Makuu ya Wizara jijini Dar es Salaam.
Rais wa Kampuni ya
Mitsubishi Hitachi Power System Ltd, Takato Nishizawa (Kushoto) na Kamishna
Msaidizi wa Umeme wa Wizara ya Nishati na Madini, Mhandisi Innocent Luoga
(Kulia) – (Walioshikana mikono), wakiwa katika picha ya pamoja na Maofisa
kutoka Kampuni hiyo na Wataalamu wa Wizara, mara baada ya kikao baina yao
kilichojadili ushirikiano katika sekta ya nishati nchini. Kikao kilifanyika Mei
12, 2015 Makao Makuu ya Wizara, jijini Dar es Salaam.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...