Halmashauri ya Mji Njombe imetoa msaada wa fedha wenye thamani ya shilingi Million tano (5,000,000/=) kwa vikundi vya Wajasiriamali vya Watu Wanaoishi na Virusi vya Ukimwi (WAVIU), ambapo fedha hizo zitatumika kuendeleza miradi mbalimbali iliyoanzishwa na iliyopendekezwa kuanzishwa na vikundi hivyo.

Mratibu wa Ukimwi katika Halmashauri ya Mji Njombe Ndugu Daniel Mwasongwe alisema, fedha hizo zimetolewa kwa lengo la kuviwezesha vikundi hivyo kuongeza kipato ambacho kitawasaidia kuendesha maisha yao ya kila siku, kuondokana na dhana ya utegemezi na kuimarisha umoja na mshikamano miongoni mwa wanakikundi.

“Halmashauri ina vikundi vingi sana vya WAVIU ambavyo vinahitaji misaada kama hii ili kuweza kukuza na kuendesha miradi yao. Lakini leo hii tumeamua kutoa msaada huu wa fedha kwa baadhi ya vikundi kutokana na ukweli usiofichika kuwa miradi yenu ipo wazi na inaonekana. Tumieni fedha hizi kuendeleza miradi ambayo ni endelevu na ambayo mmeridhia kuianzisha kama kikundi. Tutafika na kukagua ni hatua gani mmepiga baada ya kupokea msaada huu.”Alisema mratibu huyo

Jumla ya Vikundi 6 vya WAVIU kutoka katika Kata tano ndani ya Halmashauri ya Mji Njombe vimenufaika na Msaada huo. Vikundi hivyo ni pamoja na Kikundi cha Matumaini kilichopo Kata ya Uwemba ambacho kilipewa fedha Taslimu shilingi 800,000/= kwa ajili ya shughuli za ufugaji nyuki na kilimo cha viazi, Kikundi cha Muungane kutoka Kata ya Uwemba ambacho kilipewa fedha Taslimu shilingi 1,000,000/= kwa ajili ya shughuli za Ufugaji nyuki na Kilimo cha viazi, Mwongozo kutoka kata ya Njombe Mjini ambacho kilipewa shilingi 800,000/= kwa ajili ya Ufugaji Kuku wa Kienyeji, Tulindane kutoka Kata ya Kifanya Shilingi 800,000/= kwa ajili ya Ufugaji Nyuki, Kikundi cha Upendo kutoka Kata ya Mji Mwema Shilingi 600,000/= kwa ajili ya Upandaji Miti na Kikundi cha Twitange kutoka Kata ya Matola Shilingi 1,000,000/= kwa ajili ya Ufugaji wa Ngombe wa Maziwa.

Mratibu wa Ukimwi wa Halmashauri ya Mji Njombe ameiomba jamii, Asasi za Kiserikali na Zisizo za Kiserikali kujitokeza kuvisaidia vikundi hivi vya WAVIU kwa kuwapatia misaada mbalimbali popote pale Nchini na kuondokana na dhana ya Kuwanyanyapaa na kutotambua mchango wao haswa katika maswala ya Kiuchumi na Ujasiriamali.
Mratibu wa Ukimwi wa Halmashauri ya Mji Njombe Ndg. Daniel Mwasongwe (Kushoto) akihakiki kiasi cha fedha cha shilingi 600,000/= ambazo zilikabidhiwa kwa Kikundi cha Upendo. Kulia ni Mwenyekiti wa Kikundi hicho akijaza fomu ya kukiri kupokea msaada huo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...