WAZIRI wa Nishati na Madini, George Simbachawene ameiasa Kamati ya Pamoja ya Uendeshaji wa Mgodi wa TanzaniteOne, “Joint Operating Committee”-JOC kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa ili kuwanufaisha wadau wa Tanzanite katika uvunaji wa madini hayo, huku wakilinda maslahi ya mgodi huo kwa  Taifa.

 Simbachawene ametoa rai hiyo hivi karibuni wakati akizindua Kamati ya hiyo ya JOC, katika hafla iliyofanyika kwenye eneo la mgodi wa TanzaniteOne uliopo Mirerani, katika Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara.

“Suala la kulinda maslahi mapana ya mgodi huu kwa Wabia na Taifa linawezekana, iwapo Wanakamati ya JOC mtafanya kazi kama timu kwa kila mmoja kutimiza wajibu wake ipasavyo. Hivyo basi ipokeeni kazi hii na kuitekeleza kwa ari, kasi na nguvu kubwa” Alisisitiza Mh. Simbachawene.

Ameigiza Kamati hiyo ya JOC kukamilisha majadiliano ya kuboresha Mkataba wa ubia uliokuwepo baina ya STAMICO na TML kwani mabadiliko ya Mkataba huo yataleta matokeo chanya katika udhibiti na uendelezaji wa mgodi na biashara nzima ya Tanzanite kwa manufaa ya wabia wote na Taifa pia.

“Baadhi  ya vipengele vinavyohitaji kuboreshwa ni pamoja na suala la kutangaza chimbuko la Tanzanite duniani kuwa ni Tanzania; kuimarisha mazingira ya mgodi kuwa kivutio cha utalii na mafunzo; kuchangia huduma za jamii zinazozunguka mgodi na kupanda miti katika maeneo ya mgodi ili kutunza mazingira” alifafanua Mh. Simbachawene.

Kamati hiyo ya JOC ina wajumbe 6 ambao  ni Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO; Bi. Asha Jumanne Ngoma, Prof. Peter Antony Kopoka kwa upande wa STAMICO na Bwana Faisal Juma Shahbhai, Bwana Hussein Omary Gong’a  na Bwana Halfan Mpenziye Hayeshi kwa upande wa Sky Associates Ltd. Kamati hii inaongozwa na Bwana Faisal Juma Shahbhai.

Katika uzinduzi wa Kamati hiyo, Mheshimiwa Simbachawene pia aliwakumbusha wajumbe wa Kamati ya JOC kumsimamia kikamilifu mwendeshaji wa mgodi huo yaani TML ili aweze kutekeleza masharti ya mkataba wa ubia katika uzalishaji wa Tanzanite, kwa manufaa ya pande zote.

Aidha amewasisitiza wajumbe wa JOC kufanya maamuzi yenye tija katika uidhinishaji wa bajeti, kubuni mipango ya maendeleo ya mgodi; kuandaa sera za uendeshaji; kuunda kamati za ushauri kulingana na mahitaji na kuingia makubaliano ya pamoja na Kitengo cha Uangalizi na Usimamizi (Monitoring and Evaluation Unit), kuhusu mfumo wa uendeshaji mgodi, ili kuongeza uzalishaji wa tanzanite na  kukuza  soko la ndani.

Ameitaka Sky Associates kutoa nafasi za ajira kwa Watanzania bila ubaguzi na kuzingatia misingi ya utawala bora  katika uendeshaji wa mgodi huo huku wakitoa maslahi bora kwa wafanyakazi wake.
Simbachawene amesema STAMICO kwa upande wake, haina budi kuwapatia Wafanyakazi wake waliopo Mirerani vitendea kazi stahili ili wasiwe na kisingizio cha kushindwa kutekeleza majukumu yao, na ameitaka Menejimenti ya Shirika hilo ipime utendaji kazi wa wafanyakazi wake mara kwa mara ili kukuza ufanisi.

Kuhusu suala la kuboresha mahusiano mazuri na Wachimbaji wadogo, Simbachawene amesema mahusiano kati ya TanzaniteOne na Wachimbaji Wadogo yaendelee kuimarishwa, na amekiri kuitambua Kamati Maalum iliyoundwa na Kamishna wa Madini, ili kuisaidia Serikali kuweka mfumo mzuri wa uchimbaji katika mgodi huo, jambo ambalo litaepusha ajali na kupunguza migogoro baina ya wadau.

“Nazitambua changamoto za wizi na utoroshaji wa madini ya Tanzanite ambazo ni matokeo ya wadau wasio waaminifu; nichukue fursa hii kuwataarifu kuwa Serikali imefanya marekebisho ya Kifungu cha 6(4) cha Sheria ya Madini ya Mwaka 2010. Kifungu hicho sasa kinampa Kamishna wa Madini mamlaka kamili ya kutaifisha na kupiga mnada madini yanayokamatwa yakimilikiwa kinyume cha Sheria. Hivyo, wote wenye tabia ya kufanya biashara ya madini kinyume cha Sheria wajiandae kupoteza madini yao” Aliongeza kwa msisitizo Mh. Simbachawene.

Awali, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Bwana Deusdedith Magala amemshukuru Mh. Simbachawene kwa kuunda Kamati hiyo ya JOC na kuizindua rasmi, kwani itasaidia kulinda hisa za STAMICO, za Serikali na mali za mgodi, na pia kuuwezesha mgodi kufanya maamuzi makubwa na yenye tija.

Bwana Magala amesema tangu Juni 2013 STAMICO ilipoingia ubia wa umiliki wa mgodi wa TanzaniteOne na kampuni ya TML kwa uwiano wa 50:50 wa leseni ya uchimbaji wa Tanzanite, Bodi za Wakurugenzi za wabia hao wawili ndio zimekuwa zikifanya kazi kama Kamati ya JOC, jambo ambalo lilileta mzigo mkubwa wa kazi kwa bodi hizo.

Katika hafla hiyo ya uzinduzi wa Kamati ya Ushirikiano ya Mgodi wa TanzaniteOne, Mh. Simbachawene na ujumbe wake pia walikagua shughuli za uchimbaji wa Tanzanite katika mgodi wa CT, zikiwemo uchorongaji, uchotaji na utoaji wa udongo na kujionea athari za kimazingira zilizosababishwa na wachimbaji wadogo kwenye kitalu C.

Hafla hiyo ya uzinduzi wa JOC ilihudhuriwa na mwakilishi wa Kamishna wa Madini Tanzania, Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO, Wakurugenzi wa Kampuni ya Sky Associates Ltd na TML, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania (TMAA), Kamishna Msaidizi wa Madini - Kanda ya Kaskazini, Wajumbe wa Kamati ya Pamoja ya Uendeshaji (JOC) na Waandishi wa Habari.
Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene (aliyevaa miwani) akipata maelezo kuhusu uchimbaji, ndani ya shimo la mgodi wa chini (underground mine) wa TanzaniteOne wakati alipotembelea mgodi, kabla ya kuzindua Kamati ya Pamoja ya Uendeshaji mgodi huo (JOC).
 Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene (aliyekaa katikati) katika picha na Wajumbe wa Kamati ya Pamoja ya Uendeshaji “Joint Operating Committee – (JOC) ” ya mgodi wa TanzaniteOne, baada ya kuizundua Kamati hiyo mgodini hapo mwishoni mwa wiki. Kushoto kwake ni Mwenyekiti wa JOC Bwana Faisal Juma Shahbhai na kulia kwake ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO, Duesdedith Magala. Wajumbe wengine waliokaa kutoka kushoto ni Asha Jumanne Ngoma, Prof. Peter Antony Kopoka (wa tano), Bwana Hussein Omary Gong’a (aliyesimama kushoto) na Bwana Halfan Mpenziye Hayeshi (aliyesimama kulia).
Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene (mwenye overall ya Kibluu) akipata   maelezo kutoka kwa Mwenyekiti wa Kamati ya JOC, Faisal Juma Shahbhai (aliyevaa kofia ngumu ya Kibluu) kuhusu uzalishaji wa Tanzanite katika mgodi wa TanzaniteOne. Anayemsikiliza  (mwenye overall ya Kijani) ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO, Duesdedith Magala.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...