TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za Rambirambi Waziri Mkuu Mheshimiwa Mizengo Peter Kayanza Pinda, kufuatia kifo cha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma Mheshimiwa Celine Ompeshi Kombani.
“Pokea rambirambi zangu za dhati, sote kwa pamoja tumepoteza mama mchapakazi, hodari na aliyependa kushirikiana na wenzake katika kazi zake, hakika tutamkumbuka siku zote” Rais Amesema.
Rais Pia amemtumia salamu za pole mume wa marehemu Kombani, Bwana Swaleh Ahmad Pongolani, watoto, ndugu na  jamaa wa Mama Kombani.
“Nimepokea taarifa za kifo cha mama Kombani kwa huzuni kubwa, najua machungu na maumivu mliyonayo kwa kuondokewa na kiungo muhimu katika familia yenu, poleni sana, mama ni nguzo ya familia, niko nanyi katika msiba huu mzito kwenu” Rais ametuma salamu hizo kwa Mume wa Marehemu Celine, Bwana Pongolani, watoto, wajukuu na ndugu wa Marehemu mama Kombani.
Rais amesema pamoja na kwamba kifo hakiepukiki, bado ni kitu ambacho kinashtua, kuhuzunisha na kuleta unyonge mkubwa kwa wafiwa katika jamii.
Marehemu Kombani pia alikua ni mgombea ubunge wa jimbo la Ulanga Mashariki kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi, ambapo amekwisha kulitumikia jimbo hilo kwa kipindi cha miaka 10 iliyopita.
“Naungana nanyi katika kipindi hiki kigumu kumuombea Mama Kombani ili mwenyezi Mungu ampe mapumziko mema ya Milele” Rais amesema na kuwaombea wana familia na ndugu wa Marehemu “Mwenyezi Mungu awatie nguvu, awape uvumilivu na subira katika kipindi hiki”.
“Niko nanyi katika kipindi hiki kigumu kwa hali na mali, nawaomba  msijisikie wapweke” Rais amesema na kuwatakia utulivu na amani katika kipindi hiki cha msiba mkubwa kwa familia ya mama Kombani
Marehemu Mama Kombani amefariki jana tarehe 24 Septemba, 2015 nchini India ambapo alikua anapatiwa matibabu baada ya kugundulika kuwa na kansa.
Marehemu Kombani alizaliwa Juni 19, 1959 ameacha Mume, watoto watano na  wajukuu wane.
Mwili wa marehemu unatarajia kuwasili nchini kesho mchana na anatarajiwa kuzikwa Mkoani Morogoro katika shamba lake.
Mungu ailaze Roho ya Marehemu Celine Kombani mahali Pema Peponi, Amina.

Imetolewa na:
Premi Kibanga,
Mwandishi wa Habari wa Rais, Msaidizi,
Ikulu-DSM.
25 Septemba, 2015

  

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...