Na Grace Michael, Kagera

MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya umesema hautawavumilia watumishi katika hospitali ya Mkoa wa Kagera wanaojihusisha na vitendo vya kughushi nyaraka za kuchukulia dawa katika maduka ya dawa na kuusababishia Mfuko kulipa fedha ambazo hazijatumika kihalali.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko huo Bw. Michael Mhando ameyasema hayo mjini hapa wakati akizungumza na uongozi wa Hospitali ya Mkoa wa Kagera kabla ya uzinduzi wa mpango wa Madaktari Bingwa ambao wamepelekwa na Mfuko huo kutoa huduma kwa wanachama na wananchi kwa ujumla.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Bw. Michael Mhando akiongozana na Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera Nasoro Mlambila kukagua maeneo wanayofanyia kazi madaktari bingwa ambao NHIF imewapeleka katika Hospitali ya Mkoa wa Kagera. 

“Niseme tu kwamba tumekuwa tukichukua hatua mbalimbali zikiwemo za kuwaonya kwa barua na wengine kuwafutia usajili na wengine kuwafikisha mahakamani watoa huduma ambao wanajihusisha na vitendo vya udanganyifu lakini niseme kwamba kwa hospitali hii natangaza rasmi kuwa kuanzia sasa naanza kuchukua hatua kali kwa watumishi ambao watabainika kujihusisha na udanganyifu wowote,” alisema Bw. Mhando.

Alisema kuwa Mfuko unalo jukumu la kulinda fedha za wanachama wake na kuhakikisha zinatumika katika matumizi sahihi hivyo hauko tayari kuendelea kuvumilia watoa huduma ambao sio waaminifu.

“Nawaomba sana toeni huduma kwa wanachama wetu na sio kutumia vitambulisho vyao kughushi nyaraka mbalimbali zikiwemo za kuchukulia dawa katika maduka ya dawa…sisi tuko tayari kusaidia kituo chochote katika uboreshaji wa huduma zake ili wananchi wanufaike kwa ujumla na sio kikundi cha watu wachache,” alisema Bw. Mhando.
Daktari Bingwa wa Masuala ya Usingizi na Wagonjwa Mahututi Vence Sakwari akijadili jambo na mwenyeji wake katika Hospitali ya Mkoa wa Kagera kabla ya kuanza kutoa huduma kwa wagonjwa wake. 

Katika hatua nyingine aliitaka Hospitali hiyo kuangalia namna ya uboreshaji wa huduma zake hususan upatikanaji wa dawa ambao umeonekana kuwa tatizo kubwa linaloikosesha mapato hospitali hiyo.

Alisema kuwa mpaka sasa Hospitali ya Mkoa wa Kagera imekuwa ikipoteza mapato mengi kutokana na ukosefu wa dawa na vipimo ambavyo ndivyo vinaingiza fedha nyingi katika vituo vya kutolea huduma hali ambayo inakwamisha uboreshaji wa huduma.
Sehemu ya wagonjwa wakisubiri kuelezwa utaratibu wa kuwaona madaktari bingwa waliofika hospitalini hapo. 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...