Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa amesema ujenzi wa barabara za mzunguko (ring roads) zenye lengo la kupunguza msongamano wa magari katikati ya jiji la Dar es Salaam utakamilika baadae Mwezi Juni mwaka huu.
Amesema kufuatia Serikali kuanza kulipa madeni ya makandarasi amewataka makandarasi wote kurudi kazini ili kufikia lengo la Serikali la kukamilisha barabara hizo mwezi juni sambamba na ulipaji wa madeni yote.
“Tunawaomba wale wenye nyumba pembeni mwa barabara za mzunguko ambao wapo kwenye orodha ya kulipwa fidia waondoke maeneo hayo ili kuruhusu kazi ya ujenzi wa barabara kuendelea”, amefafanua Waziri Prof. Mbarawa.
Waziri Prof. Mbarawa amekagua barabara za Tankibovu - Goba (km9), Goba – Mbezi Mwisho (Km7), Kimara Baruti – Msewe - Chuo Kikuu (km2.6), Mbezi Mwisho – Malambamawili – Kifuru - Kinyerezi (km14), na Tabata Dampo - Kigogo (km1.6).
Barabara hizo zenye urefu wa Km 27.2 zimejengwa kwa gharama ya takriban sh. bilioni 56.3 ikiwa ni gharama za ujenzi na fidia ambazo zote zinalipwa na fedha za mfuko wa barabara.
Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS), Eng. Patrick Mfugale amewataka madereva kulinda barabara hizo kwa kutoegesha magari katika maeneo yasiyoruhusiwa na kukemea vitendo vya uchimbaji mchanga pembeni mwa madaraja.
Waziri Prof. Mbarawa pia amekagua ujenzi wa daraja la Kinyerezi lenye urefu wa mita 40 lililojengwa kwa gharama ya sh. Bilioni 2.3 ambao ujenzi wake umekamilika.
Barabara za mzunguko jijini Dar es Salaam zinajengwa kwa kiwango cha lami ili kuvutia magari mengi kutumia barabara hizo na kupunguza msongamano katikati ya jiji ambapo hadi sasa Km 27 zimekamilika na Km 28 zinaedelea kujengwa.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, 
Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa (wa pili kulia), akimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), Eng. Patrick Mfugale (wa tatu kulia), huku Meneja wa TANROADS mkoa wa Dar es Salaam Eng. Julius Ndyamukama akifatatilia maelezo hayo.
 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa akifafanua hatua za Serikali za kuhakikisha ujenzi wa barabara za mzunguko jijini Dar es Salaam unakamilika mwezi juni mwaka huu.
 Meneja wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), mkoa wa Dar es Salaam Eng. Julius Ndyamukama akitoa taarifa kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa ya mradi wa ujenzi wa barabara ya Kimara - Baruti – Msewe – Chuo Kikuu yenye urefu wa Km 2.6.
 Muonekano wa daraja la kinyerezi lenye urefu wa mita 40 ambao ujenzi wake umekamilika
Muonekano wa Barabara ya Tankibovu-Goba inayojengwa kwa kiwango cha Lami kama ilivyokutwa leo mchana.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...