Shirika la Majisafi na Majitaka Dar es salaam (DAWASCO), imetangaza kuwako na ongezeko la Maji katika maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es salaam, pamoja na maeneo ya miji ya Kibaha na Bagamoyo mkoani Pwani, baada ya mtambo wa Maji wa Ruvu chini kuanza kufanya majaribio ya uzalishaji wa Maji .

Akiongea na waandishi wa habari kaimu meneja uhusiano wa DAWASCO, Bi. Everlasting Lyaro, amesema kuwa kutokana na ongezeko hilo la Maji watu wengi wameanza kupata huduma ya Majisafi, na pia kumekuwepo na ongezeko la uvujaji wa Maji katika maeneo mengi ya jiji la Dar es salaam, hasa katika maeneo ambayo yalikuwa na miundombinu ya Maji lakini hayakuwa na huduma ya Maji na baadhi ya maeneo ambayo yalikuwa yakipata Maji kwa msukumo mdogo (Low pressure).

“Kufuatia ongezeko hili la Maji watu wengi wameanza kupata huduma ya Majisafi, na uvujaji wa Maji umeongezeka katika maeneo ambayo aidha yalikuwa na miundombinu ya Maji lakini hayakuwa na huduma ya Maji au maeneo ambayo yalikuwa yakipata Maji kwa msukumo mdogo” Alisema Bi. Lyaro.

Aidha, ametoa wito kwa wateja na wananchi wote kutoa taarifa za uvujaji huo wa Maji pindi wanapobaini kuwapo na uvujaji wa Maji katika makazi yao na maeneo mbalimbali ya jiji kupitia kituo cha huduma kwa wateja kwa kupiga simu namba 022194800 au 0800110064 (Bure).

“Namba hizi ziko wazi saa 24 kwa siku na mteja hatakatwa gharama yoyote akipiga simu hizi. Hivyo tunaomba wateja wetu waisaidie Dawasco kupunguza upotevu wa maji kwa kutupa taarifa za mivujo na kupasuka kwa mabomba” alisema bi Lyaro.
Kutokana na ongezeko hilo la Maji maeneo yaliyoanza kupata Maji baada ya majaribio ya mtambo huo kuwa ni Tandale,Manzese makunimula,Mwananyamala,Kinondoni mkwajuni, baadhi ya maeneo ya vingunguti,changombe,ubungo-mabibo na city centre.

Pia, DAWASCO imetumia nafasi hiyo kuwakumbusha wateja wote kulipia huduma ya Maji kwa wakati kwani watu wengi kwa sasa wameanza kupata huduma ya Majisafi na salama kutokana na kuongezeka kwa uzalishaji wa Maji katika mtambo wa Maji wa Ruvu chini, hivyo hawana budi kuyalipia ili kuepuka usumbufu wa kusitishiwa huduma ya Maji.

Kuongezeka kwa huduma ya Maji katika jiji la Dar es salaam na Mji wa Bagamoyo  kumetokana na kukamilika upanuzi wa mtambo wa Ruvu chini ulioanza mwaka 2011 hivyo kuongezeka kiasi cha uzalishaji wa Maji kutoka wastani wa lita milioni 182 hadi lita 270 kwa sasa.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 2 mpaka sasa

  1. Ni lini watu wa kinyerezi tutapata huduma ya maji safi na salama ya Dawasco?

    ReplyDelete
  2. Maeneo ya wazo hill bado hamna Maji hivyo hilo ongezeko halina impact kwetu

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...