Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema kwamba baadhi ya Watumishi wa Taasisi za Umma bado wana hofu ya kuogopa kustaafu utumishi wao wakihisi kunyemelewa na ukali wa maisha ya baadaye wakisahau kwamba maisha baada ya kustaafu yapo kama kawaida.
Alisema cha msingi kwa mtumishi anayehusika ni kujipanga mapema katika kujiandaa na harakati za kujiendesha kimaisha bila ya kutetereka mara amalizapo utumishi wake.
Balozi Seif Ali Iddi alitoa nasaha hizo wakati alizungumza na Uongozi wa Jumuiya ya Wastaafu wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania wanaoishi Zanzibar walipofika Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar kumpongeza baada ya kuteuliwa tena na Rais wa Zanzibar kuendelea kushika wadhifa aliokuwa nao.
Alisema ipo miradi mbali mbali nchini inayoweza kufanywa na wastaafu wa Taasisi za Umma katika kukidhi mahitaji yao ya kila siku badala ya kutumia ustaafu wao kuendeleza tabia ya kuomba wakati baadhi ya watumishi hao wana uwezo kamili wa kiafya.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwakumbusha Wastaafu hao wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kuweka mikakati imara itakayosaidia kupambana na changamoto zinazowakabili ndani ya Jumuiya yao ili wapate mafanikio yatakayostawisha maisha yao.
Mapema Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wastaafu wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Nd. Mohammed Ali alisema wana Jumuiya hiyo wako tayari kushirikiana na Viongozi na Wananchi katika kuelekeza nguvu zao kwenye miradi ya kuendeleza Nchi.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif ALI Iddi akisalimiana na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wastaafu wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mzee Mohammed Ali Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.
Balozi Seif akipokea salamu za pongezi kutoka kwa Viongozi wa Jumuiya ya Wastaafu wa SMT waliofika Ofisini kwake kumpongeza baada ya kuteuliwa tena na Rais wa Zanzibar Dr. Ali Mohammed Shein kuendelea kuwa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar. Picha na OMPR
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...