Na Allan Ntana, Kaliua

MKUU wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri amemwagiza Kamanda wa Polisi Mkoani Tabora Hamis Seleman na Mkuu wa wilaya ya Kaliua Hadija Nyembo kuhakikisha wanakomesha vitendo vya mauaji vinavyozidi kushamiri wilayani humo.

Agizo hilo amelitoa jana katika kikao maalumu cha baraza la madiwani wa halmashauri ya wilaya hiyo kilichofanyika katika ukumbi wa Milenia mjini Kaliua.

Alisema vitendo vya mauaji kwa raia wasio na hatia katika mkoa huo vimekuwa vikishamiri siku hadi siku vikichochewa na imani za kishirikina, wivu wa mapenzi na ugomvi wa mali huku matukio mengi yakiripotiwa kutoka katika wilaya hiyo.

Alibainisha kuwa takwimu zinaonesha mkoa huo ni miongoni mwa mikoa yenye matukio mengi ya mauaji jambo ambalo hawezi kuliacha liendelee pasipo kuchukua hatua za makusudi za kukomeshwa kwa vitendo hivyo.

‘Kamanda wa Polisi Mkoa (RPC), OCD Kaliua na Mkuu wa wilaya hakikisheni mtu yeyote atakayeua mwenzake akamatwe mara moja na afikishwe katika vyombo vya sheria’, aliagiza.

Aidha aliwaagiza madiwani, watendaji wote wa vijiji na kata kwa kushirikiana na Kamati nzima ya ulinzi na usalama ya wilaya kusimamia ipasavyo agizo hilo ili kuhakikisha matukio ya namna hiyo yote yanakomeshwa na wananchi wanaishi kwa amani.

‘Ndugu zangu hatuwezi kukubali watu wandelee kuuana kama kuku, watendaji wa vijiji na kata toeni ushirikiano katika hili, leteni taarifa za wote wanaojihusisha na vitendo hivyo kwa diwani au ofisi ya Mkuu wa wilaya ili kukomesha mauaji hayo,’ aliongeza.

Aidha RC aliwataka madiwani wa halmashari hiyo kuhamasisha wazazi wote kupeleka watoto wao shule ili wapate elimu kwa kuwa msingi mzuri wa maisha ni elimu huku akiwaagiza kuchukua hatua kwa wote watakaokaidi.

Agizo la Mwanri kukomesha mauaji katika wilaya hiyo liliungwa mkono na Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo Haruna Kasele, Mbunge wa jimbo la Ulyankulu John Kadutu, Mbunge wa jimbo la Kaliua Magdalena Sakaya na Mkuu wa wilaya hiyo.
Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri (wa tatu toka kulia) akiwa katika kikao cha baraza la madiwani wa halmshauri ya wilaya ya Kaliua jana,anayeongea katika kipaza sauti ni Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya Haruna Kasele. (Picha na Allan Ntana)

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...