Wanawake katika Halmashauri za Wilaya ya Bahi Mkoani Dodoma wakishiriki katika
zoezi la kuanisha mipaka ya maeneo yao yatakayotumika katika shughuli mbalimbali za
kijamii ikiwemo makazi, kilimo,biashara n.k lililofanyika hivi karibuni Wilayani humo.
Wananchi katika Halmashauri ya Wilaya ya Bahi Mkoani Dodoma wakifuatilia mafunzo
kuhusu mpango wa matumizi bora ya ardhi yaliyokuwa yakitolewa na Maafisa kutoka Shirika
la PELUM Tanzania hivi karibuni.
Na Mwandishi Wetu,
Kilolo
WANAWAKE katika Halmashauri za Wilaya ya Kilolo na Mufindi Mkoani Iringa
wamepongeza jitihada za Shirika la PELUM Tanzania za kuwapatia elimu ya mafunzo
kuhusu Mipango ya Matumizi bora ya Ardhi Vijijini kwa kuwa hatua itawasadia
kutambua haki walizonazo katika kumiliki, kutumia na kupata rasilimali ya ardhi.
Akizungumza hivi karibuni katika semina ya mafunzo ya mipango ya matumizi bora ya
ardhi kwa Wananchi Wilayani Kilolo, Afisa Mipango Mji na Vijiji wa Wilaya ya Kilolo,
Bernard Kajembe alisema kabla ya utekelezaji wa mradi wa CEGO suala la umiliki
ardhi hususani kwa wanawake Wilayani humo ilikuwa ni jambo lisilopewa kipaumbile.
Kajembe alisema kuwa kwa kipindi kirefu mwanamke amekuwa akikosa haki yake ya
kumiliki Ardhi kwa kigezo kuwa hana thamani kwenye familia aliyozaliwa na badala
yake thamani yake ipo kwenye familia atakayoolewa na hivyo kupelekea mwanamke
kuwa na jukumu la kutumia ardhi kwa ajili ya uzalishaji pekee.
“Tunalishukuru Shirika la PELUM Tanzania kwa kushirikiana na Halmashauri kutekeleza
mradi huu na kutoa elimu ya awali kuhusiana na masuala ya ardhi ambapo imetoa
mwanya kwa wanawake kuanza kumiliki ardhi na hasa kwenye vijiji vya mradi jambo
ambalo kwa awali lilionekana ni kama uvunjaji wa mila na desturi” alisema Kajembe.
Kwa upande wake Bi. Maliamusi Mdalingwa mkazi wa kijiji cha Ugesa Wilayani Kilolo
alisema katika siku za nyuma ilikuwa jambo gumu kwa wanawake wengi ndani ya ndoa
kumiliki hata kama ana haki ya kisheria kumiliki kwa makubaliano yao wawili.
Anasema mara baada ya mafunzo kutoka Shirika la PELUM Tanzania kwa sasa hali
imekuwa tofauti kwani anathamini hata haki za watoto wake wa kike kuwa nao
wanapaswa kumilikishwa rasilimali ya ardhi.
Naye Bi. Agnes Mbamilo toka kijiji cha Isaula wilayani Mufindi alipongeza Shirika la
PELUM Tanzania kwa kwa kuwapatia mafunzo hayo kwani yamesaidia kwa kiasi
kikubwa kubadili fikra na mtazamo wa mume wake kwa sasa wana umiliki wa hati ya
pamoja katika shamba na kiwanja cha nyumba.
Mbali na elimu ya Haki za ardhi kwa wanawake, mafunzo mengine yanayotolewa na
Shirika la PELUM Tanzania ni pamoja na elimu juu ya Mpango wa matumizi ya Ardhi
kijijini, Haki ya kupata, kutumia na kumiliki Ardhi Tanzania, Utatuzi wa Migogoro ya
Ardhi Tanzania pamoja na Utawala wa Kidemokrasia katika Jamii.
Mafunzo hayo yanatolewa kupitia mradi wa ushiriki wa wananchi kwenye Sekta ya
kilimo (CEGO) na kufadhiliwa na Shirika la Misaada la Marekani (USAID) yalitolewa
katika vijiji 10 vya Wilaya hizo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...