Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 25 Oktoba, 2017 amepokea hati za utambulisho za Mabalozi watatu waliopangiwa kuziwakilisha nchi za Oman, Uholanzi na China hapa nchini.

Waliowasilisha hati zao kwa Mhe. Rais Magufuli, Ikulu Jijini Dar es Salaam ni Mhe. Ali Abdullah Al Mahruqi – Balozi wa Oman hapa nchini, Mhe. Jeroen Verheul – Balozi wa Uholanzi hapa nchini na Mhe. Wang Ke – Balozi wa China hapa nchini.

Mhe. Rais Magufuli amewapongeza Mabalozi hao kwa kuteuliwa kuziwakilisha nchi zao hapa nchini na amewahakikishia kuwa Serikali yake itafanya kazi nao kwa ukaribu ili kuendeleza na kukuza zaidi ushirikiano kati ya nchi hizo na Tanzania hususani katika uchumi.

“Nimefurahishwa sana na ziara iliyofanywa na Mawaziri wa Oman hapa nchini, naomba ufikishe shukrani zangu kwa Mfalme wa Oman Mtukufu Sayyid Qaboos bin Said Al Said, naamini yote tuliyozungumza ikiwemo kubadilishana uzoefu katika mafuta na gesi, uwekezaji katika viwanda na ujenzi wa miundombinu tutayatekeleza kwa manufaa ya wananchi wa nchi zetu” amesema Mhe. Rais Magufuli alipozungumza na Balozi Ali Abdullah Al Mahruqi wa Oman.
Mhe. Rais Magufuli amemuambia Balozi Jeroen Verheul wa Uholanzi kuwa Tanzania inayo gesi nyingi na itafurahi kupokea wawekezaji kutoka Uholanzi ikizingatiwa kuwa nchi hiyo ina uzoefu na teknolojia kubwa katika sekta hiyo.
Kwa upande wa Balozi wa China hapa nchini Mhe. Wang Ke, Mhe. Rais Magufuli amesema uhusiano wa Tanzania na China ni wa kihistoria na kidugu, hivyo ametoa wito kwa Balozi huyo kuuendeleza na kuhakikisha fursa zenye manufaa kwa nchi zote zinatumiwa ipasavyo ikiwemo kukuza uwekezaji, biashara, utalii na ushirikiano katika usafiri wa anga. 

 Gerson Msigwa 
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, 
IKULU 
Dar es Salaam 
25 Oktoba, 2017.
  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli akipokea Hati ya utambulisho kutoka kwa Balozi wa China hapa nchini  Mhe. Wang Ke, Ikulu jijini Dar es Salaam. Katikati ni Mkuu wa Itifaki Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Grace Alfred Martin
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli akitazama vitabu alivyokabidhiwa na Balozi wa China hapa nchini Mhe. Wang Ke, Ikulu jijini Dar es Salaam.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli akipokea Hati ya utambulisho kutoka kwa Balozi wa Uholanzi hapa nchini  Mhe.  Jeroen Verheul Ikulu jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkuu wa Itifaki Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Grace Alfred Martin
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli akipokea Hati ya Utambulisho kutoka kwa Balozi wa Oman hapa nchini  Mhe. Ali Al Mahruqi Ikulu jijini Dar es Salaam. Katikati ni Mkuu wa Itifaki Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Grace Alfred Martin
BOFYA HAPA KWA PICHA ZAIDI

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...