Benki Kuu ya Tanzania inapenda kuutaarifu umma kuwa taarifa zinazosambaa mitandaoni kuhusu sekta ya kibenki nchini kutokuwa salama si sahihi na zinapaswa kupuuzwa. Sekta ya kibenki nchini ipo salama na Benki Kuu ipo makini kuhakikisha kuwa sekta ya kibenki na mfumo wa fedha kwa ujumla ni salama na stahimilivu.

 Benki Kuu inaendelea kuzisimamia benki zote kwa ukaribu kama inavyotakiwa kwa mujibu wa Sheria ya Mabenki na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006. Taarifa zinazosambaa kuhusu kufungwa kwa benki zenye viwango vikubwa vya mikopo chechefu (non-performing loans) hazina ukweli wowote. Taarifa hizo zina lengo la kupotosha umma na kusababisha taharuki kwa wananchi. Benki Kuu inawakumbusha wananchi kuwa benki ndiyo sehemu salama ya kuhifadhi fedha zao. 

Benki Kuu inapenda kuuhakikishia umma kuwa haina lengo la kufuta leseni za benki bila sababu za msingi kama inavyopotoshwa kwenye mitandao ya kijamii. Ni lengo la Benki Kuu kuona kuwa benki zote zilizopewa leseni zinafanya vizuri. Aidha, ieleweke kuwa Benki Kuu hufuta leseni ya benki pale tu benki husika inaposhindwa kuzingatia vigezo ambavyo vimewekwa kisheria. Miongoni mwa sababu za msingi zinazoweza kusababisha kufutwa kwa leseni ya benki ni kuwa na mtaji chini ya kiwango kinachotakiwa kisheria, upungufu wa ukwasi na ukiukwaji wa sheria mbalimbali za kibenki, na si vinginevyo.

 Benki Kuu itaendelea kusimamia shughuli za kibenki kwa ukaribu na kwa mujibu wa Sheria ili kuhakikisha amana za wateja zinakuwa salama muda wote. Hivyo, wananchi wanaombwa kuwa na utulivu na kuondokana na taharuki inayosababishwa na watu wachache. Pia Benki Kuu inawakumbusha wananchi kutoziamini taarifa zisizo rasmi kuhusu usalama wa sekta ya kibenki nchini Tanzania. 

Taarifa rasmi kuhusu sekta ya kibenki hutolewa na Benki Kuu ya Tanzania ambayo kisheria ndiyo msimamizi wa sekta hiyo nchini. Wananchi wanakumbushwa kuwa usambazaji wa taarifa zisizo rasmi ni kinyume cha Sheria ya Makosa ya Mtandao ya mwaka 2015 na hatua kali zitachukuliwa kwa atakayebainika kufanya hivyo.

 Imetolewa na: Idara ya Uhusiano wa Umma na Itifaki
 info@bot.go.tz
 Januari 9, 2018 
 BENKI KUU YA TANZANIA

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...