Na Lydia Churi-Geita.
Katika kutekeleza dhamira yake ya kuboresha huduma za Mahakama na kusogeza huduma hizo karibu zaidi na wananchi, Mahakama ya Tanzania kwa kushirikiana na Benki ya Dunia imeanza rasmi ujenzi wa majengo matatu ya Mahakama katika mkoa wa Geita pamoja na wilaya zake za Bukombe na Chato.
Ujenzi wa Mahakama hizi ni utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Miaka Mitano (2015/16 hadi 2019/2020) wa Mahakama ya Tanzania pamoja na Mradi wa Maboresho ya Huduma za Mahakama ambao ulianza kutekelezwa rasmi mwaka 2015. Miradi hii kwa pamoja inalenga kuboresha huduma na kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi.
Mahakama imeanza ujenzi wa jengo la Mahakama ya Mkoa wa Geita ambalo litajumuisha pia na Mahakama ya wilaya ya Geita. Majengo mengine yanayojengwa ni ya Mahakama za wilaya za Bukombe na Chato.
Majengo haya yanatarajiwa kukamilika katika kipindi cha miezi sita kutoka sasa na yanajengwa kwa kutumia teknolojia ya kisasa na gharama nafuu na ya muda mfupi iitwayo Moladi ambapo kampuni ya Moladi Tanzania ndiyo imepewa dhamana ya kujenga majengo hayo. Jumla ya majengo ya Mahakama za Mkoa, wilaya na Mwanzo sita tayari yameshajengwa kwa kutumia teknolojia ya Moladi katika jiji la Dar es salaam na Mkoa wa Pwani.
Jengo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Geita na Mahakama ya Wilaya Geita likiwa katika hatua za awali za ujenzi 
Jengo la Mahakama ya Wilaya ya Bukombe likiwa katika hatua za awali za ujenzi wake katika mji mdogo wa Ushirombo wilayani Bukombe.
Jengo la Mahakama ya wilaya ya Chato likiwa katika hatua ya Msingi. Majengo haya yote yanajengwa kwa Teknolojia ya Gharama nafuu na ya muda mfupi iitwayo Moladi na yanajengwa na Kampuni ya Moladi Tanzania. Ujenzi wake unatarajiwa kutumia muda wa miezi sita.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...