NA TIGANYA VINCENT
MKUU wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri amemwagizwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua kumchukua hatua Afisa Ugani wa Kata ya Sasu Amos Kafulila kwa kosa la kutokuwepo katika Kituo chake cha kazi bila ruhusa.
Alisema hatua hiyo inakwenda kinyume cha agizo la Mkoa la kuwataka watumishi wote wanaohusika na Kilimo kuwa karibu na wakulima kipindi hiki cha msimu wa kilimo ili kuwasaidia kulima kilimo cha kisasa. Mwanri alitoa agizo hilo juzi katika Kata ya Sasu wilayani Kaliua wakati wa ziara yake ya kikazi ya kuhamasisha kilimo bora ikiwemo kilimo cha pamba kwa kuzingatia Sheria na kununi 10 za zao hilo na kumkuta hayupo katika Kituo chake cha kazi.
Alisema Ofisi ya Mkoa ilishatoa maelekezo kuwa Maofisa Ugani wote katika kipindi hiki cha kilimo ,likizo zao zitaharishwa hadi hapo baadaye ili waende vijijini kuwasaidia wakulima kulima kilimo chenye tija , lakini wapo baadhi yao wamekaidi na kuondoka katika maeneo yao bila hata kutoa taarifa kwa viongozi jambo ambalo ni utovu wa nidhamu. Mwanri alisema mkulima ni lazima asaidiwe kuondokana na kilimo cha kizamani cha kupata chakula cha kujikimu na badala yake azalishe ziada kwa ajili ya maendeleo yake na ujenzi wa viwanda nchini.
Alisema kimsingi Ofisi ya Mkoa haijazuia likizo ilichofanya ni kusogeza mbele ili Maofisa Ugani na watumishi wanaohusika na kilimo watumie kipindi hicho cha kilimo kuwasaidia wakulima kukabiliana na matatizo yanayorudisha nyuma maendeleo yao. Mwanri alisema Afisa Kilimo hakuajiriwa kukaa Ofisini bali ni kwenda kwa wakulima na kuwafundisha na kuwaelekeza mbinu sahihi za kilimo.
Alisema Afisa Ugani ambaye atakuwa na matatizo ambayo yanahitaji ruhusu ni lazima aombe kwa Mkurugenzi Mtendaji wake na kisha Mkuu wa Wilaya husika na Mkoa ufahamishe na sio kuondoka bila mamlaka ya juu kupewa taarifa.

Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri(kushoto) akitoa ushauri jana kwa Mwenyekiti wa Halmashauri wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua Haruna Kasele(kulia) juu ya kuunga mkono juhudi za wakazi wa kijiji cha Miti mitano za ujenzi wa Shule ya Msingi .Katikati ni Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo Dkt. John Pima.


Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...