Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)  Prof. Mohamed Janabi akizungumza na wafanyakazi wa Taasisi hiyo katika kikao cha kufungua mwaka  kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam.
 Mkuu wa Kitengo cha Ununuzi na Ugavi wa  Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) CPSP Bunare Daniel  akielelezea umuhimu wa kufuata sheria za manunuzi katika kikao cha  kufungua mwaka cha wafanyakazi wa Taasisi hiyo kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam.
 Mwimbaji wa nyimbo za Injili na  mfanyakazi  wa  Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dorothy Nyanda akiwaeleza wafanyakazi wenzake kuhusu albamu yake mpya iitwayo Kristo Seba Waajuka (Bwana Yesu amefufuka) aliyoizindua mwishoni mwa mwaka jana akiwa na malengo ya  nusu ya mauzo ya albamu hiyo kutumika kulipia gharama za matibabu ya moyo kwa watoto ambao familia zao hazina uwezo  wakati wa  kikao cha  wafanyakazi wa Taasisi hiyo kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam.
 Mkuu wa Idara ya  Rasilimali watu wa  Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)  Ghati Chacha akijibu swali  kuhusu upandishwaji wa vyeo kwa wafanyakazi katika kikao cha  wafanyakazi wa Taasisi hiyo kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam.
 Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Afya na Serikali kuu  (TUGHE) tawi la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Godfrey Tamba akiushukuru uongozi wa Taasisi hiyo kwa kusimamia maslahi ya wafanyakazi wakati wa  kikao cha  wafanyakazi wa Taasisi hiyo kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam. Kulia ni Afisa Muuguzi wa JKCI  Oliver Marandu.
  Kaimu Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Utawala na Fedha wa  Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)  CPA Mohamed Songoro akisoma taarifa ya utendaji kazi wa kurugenzi hiyo katika kikao cha  wafanyakazi wa JKCI  kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam.
 Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Upasuaji wa  Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)  Dkt. Angela Muhozya akisoma taarifa ya utendaji kazi wa kurugenzi hiyo katika kikao cha  wafanyakazi wa JKCI  kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam.




  Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakimsikiliza   Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Prof. Mohamed Janabi (hayupo pichani) wakati wa kikao cha kufungua mwaka  cha wafanyakazi hao kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam.


Na Mwandishi Maalum - Dar es Salaam 
 TAASISI ya Moyo Jakaya Kikwete kwa mwaka wa 2020 imejipanga kufanya upasuaji wa mishipa ya damu na mapafu, upasuaji wa moyo wa kufungua na bila kufungua kifua kwa wagonjwa 2140. 

Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Prof. Mohamed Janabi katika kikao cha kufungua mwaka cha wafanyakazi wa JKCI kilichofanyika jijini Dar es Salaam. 

Prof. Janabi alisema idadi ya wagonjwa wanaosubiri kufanyiwa upasuaji mkubwa wa kusimamisha moyo, upasuaji wa bila kufungua kifua pamoja na upasuaji wa mishipa ya damu na mapafu ni kubwa hivyo basi Taasisi hiyo imejipanga kuhakikisha wagonjwa hao wanapata matibabu kwa wakati. 

“Kwa mwaka huu wa 2020 tumejipanga kufanya upasuaji mkubwa wa kusimamisha moyo kwa wagonjwa 400 kati ya hawa watu wazima watakuwa 250 na watoto 150. Pia tutafanya upasuaji wa mishipa ya damu na mapafu kwa wagonjwa 240”,. 

“Kwa upande wa upasuaji wa bila kufungua kifua kupitia tundu dogo linalotobolewa kwenye paja kwa kutumia mtambo wa Cathlab (Catheterization laboratory) tumejipanga kufanya upasuaji kwa wagonjwa 1500 kati ya hawa watoto ni 96 na watu wazima 1404”, alisema Prof. Janabi. 

Mkurugenzi huyo Mtendaji ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo alisisitiza kwa kusema kuwa idadi hiyo ya wagonjwa inaweza kamilika kama watafanya kazi kwa kujituma, ushirikiano na kufuata maadaili ya kazi. 

Aidha Prof. Janabi aliwasihi wafanyakazi wa Taasisi hiyo kuwaelimisha wagonjwa pamoja na ndugu zao ili waweze kujiunga na mifuko ya bima za afya kwa kufanya hivyo wataweza kuepukana na gharama za matibabu kwani wagonjwa wengi wanaotibiwa katika Taasisi hiyo wanatoka katika familia maskini na hivyo kushindwa kulipia gharama za matibabu. 

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Afya na Serikali kuu (TUGHE) tawi la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Godfrey Tamba aliushukuru uongozi wa Taasisi hiyo kwa kusimamia maslahi ya wafanyakazi na kuahidi wataendelea kufanya kazi kwa bidii ili kuendeleza huduma zinazotolewa na Taasisi hiyo. 

Kwa mwaka 2019 Taasisi hiyo ilifanya upasuaji wa moyo kwa wagonjwa 1873 na kuokoa zaidi ya shilingi bilioni 28 fedha ambazo Serikali ingezilipa kama wagonjwa hao wangetibiwa nje ya nchi. 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...