Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imesaini makubaliano na Wizara ya Kilimo kwa ajili ya kutekeleza mradi wa Kudhibiti Sumukuvu nchini Tanzania, kwa Kiingereza "Tanzania Initiatives for Preventing Aflatoxin Contamination (TANIPAC)".
Makubaliano hayo yametiwa saini leo kati ya Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt. Pancras Bujulu na Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Mhandisi Mathew Mtigumwe, aliyewakilishwa kwenye hafla hiyo na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Kilimo, Bi. Hilda Kinanga.
Jukumu la VETA katika mradi wa TANIPAC ni kutoa mafunzo kwa vijana 400 katika kutayarisha vihenge vya chuma (metal silos) kwa ajili ya kuhifadhia mazao.
Mradi huo utakaotekelezwa kwa miaka mitano, kuanzia 2019 hadi 2023 unalenga kushughulikia changamoto ya usalama wa chakula, hususani Sumukuvu, katika mnyororo wa thamani wa mazao ya karanga na mahindi.
Akizungumza baada ya kutia saini makubaliano hayo, Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt. Bujulu, amesema VETA imelipokea jukumu hilo kama fursa ya kipekee, kwani ingawa imekuwa ikitoa mafunzo kwenye fani mbalimbali za kilimo, ni mara ya kwanza kupewa jukumu maalum kwa ajili ya mafunzo ya utengenezaji wa vihenge (silos).
_“Tuko tayari kutoa mafunzo hayo kwa hao vijana 400 waliolengwa na mradi huu ambao watakuwa chachu katika kusambaza teknolojia hiyo nchini. Lakini hatutaishia hapo tu, bali tutatoa kwa Watanzania wengine watakaohitaji mafunzo hayo ili kusaidia kulinda afya za walaji na kuongeza tija kwenye kilimo,”_ Dkt. Bujulu amefafanua zaidi.
Kwa upande wake Bi. Kinanga ameishukuru VETA kwa kukubali ushirikiano huo na kueleza kuwa ana matumaini kuwa ushirikiano huo utaweza kuleta matokeo yaliyotarajiwa.
Mkurugenzi Mkuu wa VETA Dkt. Pancras Bujulu (katikati) akitia saini makubaliano ya kutekeleza mradi wa Kudhibiti Sumukuvu nchini Tanzania (TANIPAC) unaotekelezwa kwa pamoja na VETA na Wizara ya Kilimo. Kushoto ni Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Kilimo, Bi. Hilda Kinanga aliyemwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Mhandisi Mathew Mtigumwe na kulia ni Mwanasheria wa VETA Peter Mnyeshi.
Mkurugenzi Mkuu wa VETA Dkt. Pancras Bujulu (katikati) na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Kilimo, Bi. Hilda Kinanga wakipeana mikono ya kupongezana baada ya kutia sanini makubaliano ya kutekeleza mradi wa Kudhibiti Sumukuvu nchini Tanzania (TANIPAC).
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...