Na Leandra Gabriel, Michuzi TV
JESHI
 la Magereza limeeleza kusikitishwa na kitendo cha viongozi wa Chama cha
 Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kwa kushindwa kutii sheria bila 
shuruti na kuhatarisha usalama wa wafungwa, askari na mali za Jeshi la 
Magereza na hiyo ni baada ya watu wanaoaminika kuwa ni wafuasi na 
viongozi wa chama hicho wakiwa katika msururu ya magari binafsi na gari 
za kubeba abiria kufika katika eneo la gereza la Segerea na kutaka 
kuingia bila utaratibu.
Taarifa
 iliyotolewa na msemaji wa Jeshi la Magereza SSP Amina Kavirondo 
imeeleza kuwa Jana Machi 13, 2020  viongozi wa CHADEMA wakiwa na wafuasi
 wao walifika eneo la Magereza wakiwa na makundi ya watu na msururu wa 
magari binafsi na magari ya kubeba abiria na walipofika geti kuu 
walitaka kuingia ndani na magari yao jambo ambalo ni kinyume na taratibu
 za kiusalama katika eneo hilo ambalo limezuiliwa.
Taarifa
 hiyo imeeleza kuwa Askari wa Jeshi la Magereza waliokuwa zamu 
walijaribu kuwasihi watu wao na kuwaeleza kuwa ni mtu mmoja tuu 
anayetakiwa kuingia ndani na kukamilisha utaratibu wa kumtoa mfungwa 
aliyelipiwa faini lakini jitihada hizo za kufafanua utaratibu 
hazikusaidia na watu hao walikaidi na kuendelea kuweka msongamano katika
 eneo hilo la kiusalama na kutoa maneno ya kashfa, matusi, vitisho na 
kumshambulia askari aliyekuwepo zamu na kumchania sare za Jeshi la 
Magereza.
Imeelezwa kuwa 
utaratibu wa kusimamia usalama wa eneo la Magereza na itifaki za 
kiusalama magerezani zilifuatwa na watu hao kuondolewa kwa nguvu ya 
wastani hadi nje ya eneo la Magereza.
Pia
 taarifa hiyo imeeleza umma wa watanzania kuwa utaratibu unaotumika 
kufika na kutembelea maeneo ya Magereza ikiwa ni kwa lengo la kuona 
wafungwa au kuwatoa wafungwa waliomaliza adhabu yao utaratibu huanzia 
mahakamani kwa kulipa faini  na mahakama kutoa hati ya uthibitisho wa 
kupokea malipo hayo hatimaye hati hiyo kukabidhiwa kwa mkuu wa gereza 
ambaye hufuata taratibu na itifaki ya gereza na kumtoa mfungwa 
aliyemaliza Kifungo.
Pia 
imeelezwa kuwa wananchi lazima wafuate kanuni na Sheria za maeneo hayo 
nyeti ya kiusalama yaliyozuiliwa kwa kutofanya mambo yaliyozuiliwa 
ikiwemo kutoingia na simu au kamera, kupiga picha, kupiga kelele na 
kuweka mikusanyiko.
Jeshi
 hilo limetoa Rai na onyo kali na kueleza kuwa halitovumilia vitendo vya
 mtu au kundi lolote litakalokaidi Sheria, kanuni na miongozo ya 
utendaji kazi wa jeshi  na limetoa pongezi kwa wananchi wote wanaotii 
sheria bila shuruti na kuwakaribisha kuendelea na kupata huduma ambazo 
jeshi la Magereza linatoa.
Msemaji wa Jeshi la Magereza SSP Amina Kavirondo 



Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...