Na Karama Kenyunko, globu ya jamii
FUNDI Simu, Said Msangi (30) na mfanyabiashara Abdul Nassoro( 36), wakazi wa jijini Dar es Salaam wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na makosa matatu likiwemo la kujihusisha na simu zilizofungwa huku wakijua ni kinyume cha sheria.
Washtakiwa hao wamesomewa mashtaka yao leo Machi 11, 2020 mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Augustina Mmbando.
Akisoma hati ya mashtaka wakili wa Serikali Easter Martin amedai Februari 27, mwaka huu huko katika eneo la barabara ya Agrey mtaa wa Kariakoo, Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam walikula njama ya kutenda kosa la kujaribu kuingilia namba tambulishi ya simu.
Katika shtaka la pili, imedaiwa siku na mahali hapo hapo washtakiwa hao kwa makusudi, walijaribu kubadili namba tambulishi ya Tecno 354213067976598 na 354213067923426.
Katika shtaka la tatu, imedaiwa Nassoro na Msangi walijihusisha na simu zilizofungwa, ambapo kwa makusudi na kinyume cha sheria walifungua namba za simu zilizofungwa kwenda kwenye IMEI (354213067976598 na 354213067923426) ili kuweza kupoteza uhalisia.
Hata hivyo washtakiwa wote wamekana kuhusika na tuhuma hizo na wamerudishwa rumande kwa baada Ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana na Wakili Easter alidai upelelezi haujakamilika na kuomba tarehe nyingine ya kutajwa.
Hakimu Mmbando amesema ili washtakiwa wawe nje kwa dhamana, kila mshtakiwa anatakiwa awe na wadhamini wawili watakaosaini bondi ya Sh. milioni tano na pia mdhamini mmoja atatkiwa awe na barua inayotoka katika ofisi inayotambulika.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...