Afisa Muuguzi wa chumba cha upasuaji kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Aimana John akiwaelekeza wauguzi wenzake namna sahihi ya kunawa mikono kwa maji safi yanayotiririka na sabuni wakati wa mafunzo ya jinsi ya kupambana na ugonjwa wa Corona (COVID-19) yanayotolewa kwa wafanyakazi wa Taasisi hiyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akizungumza na Wauguzi wa Taasisi hiyo walioshiriki mafunzo ya jinsi ya kupambana na ugonjwa wa Corona (COVID-19) yanayotolewa kwa wafanyakazi wa Taasisi hiyo. Lengo la mafunzo hayo ni kuwafanya wafanyakazi wa Taasisi hiyo kuufahamu vizuri ugonjwa wa Corona na kufahamu njia za kuzifuata ili wasipate maambukizi na wasiwaambukize wengine.
Picha na JKCI
********************************
Na Mwandishi Maalum – Dar es Salaam.

01/05/2020 Utoaji wa mafunzo ya mara kwa mara ya jinsi ya kupambana na  ugonjwa wa Corona  (COVID-19) kwa wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) umewasaidia kuelewa namna ya kujikinga na ugonjwa huo  na kuwahudumia wagonjwa bila ya kupata maambukizi.

Mafunzo hayo ambayo yamekuwa yanatolewa  kwa wafanyakazi wa Taasisi hiyo tangu ugonjwa huo ulipotangazwa hapa nchini mwanzoni mwa mwezi wa tatu mwaka huu yamewasaidia  kutokuwa na hofu na kuendelea kutoa huduma ya matibabu kwa wagonjwa wanaotibiwa katika Taasisi hiyo kiufanisi zaidi.

Hayo yamesemwa jana  jijini Dar es Salaam  na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Prof. Mohamed Janabi wakati akizungumza na baadhi ya wafanyakazi wa Taasisi hiyo waliohudhuria  mafunzo hayo.

Prof. Janabi alisema baada ya wafanyakazi wa JKCI kupewa mafunzo wameweza  kuufahamu vizuri ugonjwa wa Corona, kufahamu njia za kuzifuata ili wasipate maambukizi na wasiwaambukize wengine na  kuondoa unyanyapaa kati yao na wagonjwa kwani ugonjwa wa Corona hauchagui unaweza kumpata mtu yeyote.

“Katika mafunzo tunayoyatoa kwa wafanyakazi wetu tunawafundisha jinsi ya kuwahudumia wagonjwa kipindi hiki Kkigumu ambacho Dunia inapambana na janga la ugonjwa wa Corona. Kwani baadhi ya  dalili za ugonjwa huu zinafanana na magonjwa ya  moyo ambazo ni kushindwa kupumua  na kukohoa  hivyo basi wakifahamu jinsi ya kujikinga kutawasaidia  kuepuka kupata maambukizi’’, alisema Prof. Janabi.

Mkurugenzi huyo Mtendaji alisema ili kuwalinda wafanyakazi wa Taasisi hiyo  wasipate maambukizi wamefunga  mashine ya kutakasa mwili, wametoa vitakasa mikono pamoja na barakoa kwa wafanyakazi wote  pamoja na kuwapima joto la mwili .

Aidha kwa wataalamu wa afya ambao wanawahudumia wagonjwa wanaohisiwa kuwa na ugonjwa wa Corona wanavaa vifaa kinga  na kufuata mwongozo wa kuzuia maambukizi wa mwaka 2018 na wa uzuaiaji wa maambukizi ya Virusi vinavyosababisha ugonjwa wa Corona (COVID-19) wa  mwezi wa kwanza mwaka 2020 wakati wanawahudumia wagonjwa hao.

Prof. Janabi alisema, “Wagonjwa wanaofika kutibiwa katika  Taasisi yetu wanapimwa joto la mwili kabla ya kuanza kupata huduma ya matibabu pia tumefunga mabomba ya maji pamoja na kuweka vitakasa mikono katika maeneo mbalimbali ya Taasisi yetu hii inawafanya kupata nafasi ya kunawa mikono mara kwa mara”,.

“Tunatoa elimu ya ugonjwa huu kwa wagonjwa na ndugu wa wagonjwa  kupitia vipindi mbalimbali vinavyorushwa katika Televisheni zilizopo katika Taasisi yetu pia wataalamu wetu wanatoa elimu kila siku kabla ya kuanza kwa kliniki  zetu’’,.

Prof.Janabi aliongeza kuwa Taasisi hiyo imetenga wodi maalum kwa wagonjwa wanaohisiwa kuwa na dalili za ugonjwa wa Corona ambao baada ya majibu ya vipimo kutoka na kubainika kuwa na ugonjwa huo wanapelekwa katika kituo cha Amana na kuendelea  kupewa huduma za matibabu ya moyo wakiwa huko.

Kwa upande wake mratibu wa mafunzo hayo ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha utafiti na mafunzo  Dkt. Naiz Majani alisema kuwepo kwa mafunzo hayo kumesaidia kwa kiasi kikubwa kuwaondoa hofu wafanyakazi wa Taasisi hiyo kuhusu ugonjwa wa Corona.

Dkt. Naiz ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto alisema mafunzo hayo yanatolewa katika vikundi vichache vya wafanyakazi kutokana na kada zao hali ambayo inawasaidia kuelewa zaidi.

“Katika Taasisi yetu tuna wafanyakazi wa kada ya afya na ambao siyo wa kada ya afya, hata  mafunzo tunayoyatoa tumewagawa kutokana na kada zao na  lugha tunayotumia kufundishia ni tofauti hii yote tunataka wauelewe kwa undani zaidi ugonjwa huu na jinsi ya kujikinga wao na kuwakinga wengine wanaowazunguka”, alisema Dkt.Naiz.

Daktari huyo bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto aliwaomba washiriki wa mafunzo hayo kutoa elimu waliyoipata kwa watu wengine ili wajikinge na ugonjwa huo. Pia wafuate maelekezo yanayotolewa na wataalamu wa afya ambayo ni kuvaa barakoa, kunawa mikono mara kwa mara kwa maji safi yanayotiririka na sabuni , kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima na kukaa umbali wa zaidi ya mita moja kati ya mtu na mtu.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...