WANUFAIKA wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini wanaopokea ruzuku inayotolewa na Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) wamekumbushwa wajibu wa kuboresha maisha yao kwa kutumia vizuri fedha za ruzuku wanazopatiwa ili kuondokana na umaskini.
Akiwa katika ziara ya kikazi kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini katika Kijiji cha Kinamagi Wilayani Uyui, Mkoa wa Tabora, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi amewaasa wanufaika kutotumia kwa anasa ruzuku inayotolewa na TASAF na badala yake waitumie katika shughuli za maendeleo kama kilimo, ufugaji na ujasiriamali.
Mhe. Ndejembi amefafanua kuwa, ni wajibu wa kila mnufaika kuhakikisha anajiinua kiuchumi
kupitia fedha inayotolewa na TASAF, kwani Serikali kwa upande wake inaendelea
kutekeleza wajibu wake na maelekezo ya Mheshimiwa Rais ya kuziwezesha kaya zote
maskini nchini kupitia utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini.
Mhe. Ndejembi amewataka wanufaika wa TASAF kutosita kujikwamua katika umaskini kwa kuhofia kuondolewa kwenye Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini, na badala yake wajisikie fahari kuondokana na umaskini na hatimaye kuwa mfano bora wa kuigwa na wanufaika wengine ambao hawakutumia vema ruzuku inayotolewa na TASAF.
Aidha, Mhe. Ndejembi amezitaka Serikali za Vijiji kuacha kudai tozo ndogo ndogo kama za ujenzi wa shule siku ambayo wanufaika wanapokea ruzuku, kwani tozo hizo zinawakwamisha wanufaika kutumia ruzuku wanayoipata kwa ajili ya shughuli zitakazowasaidia kujiondoa katika umaskini.
Sanjali na hilo, Mhe. Ndejembi amewataka Watendaji wa Vijiji na Kata kutokata ruzuku za wanufaika kwa ajili ya kuchangia huduma za Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) kwani wanakwamisha jitihada za wanufaika kuboresha maisha yao, hivyo amewataka kuwaacha wanufaika wazalishe fedha ndipo wachangie huduma za mfuko huo.
Mara baada ya kuzungumza na Wananchi na wanufaika wa TASAF katika Kijiji cha Kinamagi, Mhe. Ndejembi aliwatembea wanufaika ili kujionea maendeleo waliyoyapa na hatimaye kushuhudia maendeleo ya Bi. Enviolatha Gerald Kamage ambaye ametumia vizuri ruzuku kununua cherehani, kujenga nyumba, kununua sola na kuweka umeme wa REA.
Mhe. Ndejembi ameshuhudia pia, maendeleo ya mnufaika wa TASAF, Bi. Zena Hussein Maganga ambaye amefanikiwa kutumia vema ruzuku kwa kufuga mbuzi, kuku, kununua mbolea kwa ajili ya kilimo ikiwa ni pamoja na kununua sola inayowawezesha watoto wake kujisomea wakati wa usiku.
Madhumuni
ya utekelezaji wa Mpango wa Kuzinusuru Kaya Maskini nchini ni kuziwezesha kaya
hizo kuboresha maisha kwa kuongeza kipato, fursa na uwezo wa kugharamia
mahitaji ya msingi kama vile chakula, mavazi, malazi, huduma za afya na
mahitaji ya wanafunzi shuleni.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...