NA YEREMIAS NGERANGERA..NAMTUMBO
Diwani wa kata ya Likuyu wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma ,Kassimu Gunda amekasirishwa na kitendo cha baadhi ya wananchi kumwekea jeneza usiku wa manane mwalimu Mkuu wa shule ya msingi Mfuate nyumbani kwake.
Bwana Gunda alipata taarifa kwa njia ya simu na alfajiri aliondoka na kufika katika nyumba ya mwalimu huyo na kulikuta jeneza lililokuwa linawekwa msikitini limebebwa na kuwekwa mbele ya mlango wa nyumba ya mwalimu huyo.
Gunda aliamuru jeneza hilo kurudishwa msikitini na kuitisha kikao cha wazee wa kijiji hicho pamoja na kamati ya shule kujadili kitendo cha baadhi ya wananchi kumwekea jeneza mwalimu mkuu wa shule ya msingi Mfuate na kuibua taharuki kwa walimu.
“Walimu hawa ndio wanaonisaidia mimi diwani kutekeleza ilani ya chama cha mapinduzi ya kuhakikisha wanafunzi kutoka awali mpaka darasa la saba wa shule ya Mfuate wanapata elimu ,na ili walimu hao wafundishe vizuri na kutekeleza ilani ya chama wanahitaji kupata utulivu katika kazi ya kufundisha “alisema diwani huyo.
Mwalimu mkuu wa shule hiyo bwana Peter Haule kwa upande wake pamoja na kumshukuru diwani wa kata hiyo namna alivyompa ujasiri wa kuliona tukio hilo kama ni changamoto katika maisha lakini kabla ya kuja diwani huyo alisema akili haikuwa vizuri hasa akilitazama lile jeneza na alitamani kufunga mizigo yake na kwenda ofisi ya mkurugenzi .
Kitendo cha diwani mwenyewe kushirikiana na baadhi ya wananchi kuliondoa jeneza kutoka nyumbani kwake na kufanya vikao na wazee wa kijiji hicho pamoja na kamati ya shule na kumthibitishia kuwa wananchi waliofanya hivyo wenda ni vijana wahuni na kumthibitishia usalama wake alipata faraja na kupunguza mawazo aliyokuwa nayo awali .
Kwa mujibu wa diwani zoezi la kuwapata vijana au wananchi waliofanya kitendo hicho cha kumwekea mwalimu jeneza mlangoni kwenye nyumba anayoishi wamepewa wazee wawili wa kijiji hicho ambao hakuwataja majina yao na mara watakapopatikana hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao ili kudhibiti tabia za ovyo wanazofanyiwa walimu.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...