Charles James, Michuzi TV
KAIMU Katibu wa CCM Wilaya ya Dodoma Mjini, Diana Madukwa ameliagiza Jiji la Dodoma na Meneja wa Soko la Ndugai kuhakikisha wanatatua kwa haraka changamoto zinazosababisha wafanyabiashara wasihamie kwenye soko hilo.
Madukwa ametoa agizo hilo wakati wa ziara ya kamati ya siasa ya wilaya ambapo walitembelea soko hilo kubwa jijini Dodoma na kueleza kutoridhishwa na uendeshaji wake kwani umekua siyo rafiki kwa wafanyabiashara wengi.
Amesema Serikali imetumia fedha nyingi kulijenga soko hilo lakini kumekuepo na ubabaishaji mwingi na hivyo kuagiza kuwepo kwa mazingira rafiki kwa wafanyabiashara ili waweze kuhamia hapo kufanya biashara zao zitakazowaingia mapato na kuingizia serikali kodi.
" Haiwezekani Serikali yetu ya CCM inayoongozwa na Mzalendo Dk John Magufuli inajenga soko kubwa na la heshima hapa halafu viongozi mliopewa dhamana ya kulisimamia mnashindwa kuweka mazingira rafiki kwa wafanyabiashara kuhamia hapa, tunataka tukirudi tena hapa kukagua tusikute huu ubabaishaji, hawa wafanyabiashara ndio wapiga kura wa Chama chetu na ndio waliomchagua Rais Magufuli hatutaki kuona wanakwazika," Amesema Diana Madukwa.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Dodoma Mjinu, Meja Mstaafu Johnick Risasi ameushauri uongozi wa Jiji la Dodoma juu ya ushirikishwaji kwani ni muhimu ili kuwa na kauli moja siyo Kila Mkuu wa Idara anatoa kauli yake mwisho wa siku wananchi wanakua hawaelewi lipi ni sahihi na lipi siyo sahihi.
Kamati hiyo ya siasa pia imetembelea Kituo Kikuu cha Mabasi na kushangaa kwanini mpaka sasa wamiliki wa mabasi wanaendelea kuwa na vituo vya vya mabasi wakati serikali imejenga stendi kubwa na ya Kisasa na kusema hiyo ni ishara ya kuhujumu miradi hiyo ya serikali na kuwataka wenye mamlaka kufuatilia jambo hilo.
Kaimu Katibu wa CCM Wilaya ya Dodoma Mjini, Diana Madukwa akitoa maagizo kwa uongozi wa Soko la Ndugai baada ya kutoridhishwa na usimamizi wa soko hilo.
Kamati ya Siasa ya Wilaya ya Dodoma Mjini ikiwa ndani ya Stendi Kuu ya Mabasi jijini Dodoma kukagua uendeshaji wake ambapo wameeleza kutoridhishwa na usimamizi wa stendi hiyo.
Kaimu Katibu wa CCM Wilaya ya Dodoma Mjini akitoa maelekezo kwa viongozi wa Jiji la Dodoma kwenye ziara ya kamati ya siasa ya Wilaya hiyo ya kukagua miradi mbalimbali ya serikali.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...