Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akisisitiza umuhimu wa Mpango wa Kurasimisha Rasiliamli na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) katika kuleta ukombozi wa kiuchumi na kuondoa migogoro ya ardhi visiwani Zanzibar wakati Wajumbe wa Kamati ya Uongozi ya Mpango huo (Hawapo pichani) walipomtembelea   Ikulu Jijini Zanzibar leo Februari 11, 2021 na kueleza hatua iliyofikiwa katika urasimishaji ardhi na biashara  visiwani humo.

Wajumbe wa  Kamati ya Uongozi ya Mpango wa kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) wakifuatilia hotuba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi  walipomtembelea Ikulu Jijini Zanzibar na kufanya naye mazungumzo kuhusu hatua iliyofikiwa katika urasimishaji ardhi na biashara visiwani humo.

Mratibu wa Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge  Tanzania (MKURABITA) Dkt. Seraphia Mgembe akieleza kuhusu namna wananchi wa Zanibar wanavyounga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi  Zanzibar katika kuwaletea ukombozi wa kiuchumi ikiwemo kuwezesha urasimishaji ardhi na biashara unaofanywa kupitia MKURABITA.

Makamu  Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ya Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge  Tanzania (MKURABITA) Bi. Immaculata Senje akieleza mikakati ya mpango huo ikiwemo kupima viwanja 5700, kujenga vituo jumuishi  vya Biashara vipatavyo  10 katika wilaya mbalimbali za Unguja na Pemba wakati wajumbe wa Kamati hiyo walipomtembelea Ikulu Jijini Zanzibar leo Februari 11, 2021 na kueleza utekelezaji wa Mpango huo tangua kuanza kwa shughuli za urasimishaji visiwani humo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akiwa kwenye picha ya pamoja na Kamati ya Uongozi ya Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge  Tanzania (MKURABITA), Watumishi na Menejimenti ya Mpango huo  leo Ikulu Jijini Zanzibar mara baada ya kukutana na Kamati hiyo.


Na Mwandishi Wetu- Unguja

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi amesema kuwa Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) una mchango mkubwa katika kujenga uchumi na kuondoa migogoro ya ardhi baada ya urasimishaji.

Ameyasema hayo leo Februari 11, 2021 Ikulu Jijini Zanzibar wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na wajumbe wa Kamati ya Uongozi ya MKURABITA na Menejimenti  ya Mpango huo.

"Nimejulishwa kuwa Mpango huu tangu uanze hapa Zanzibar, tayari shilingi milioni 441 zimetolewa kuwezesha urasimishaji, naahidi kwamba Serikali ya Mapinduzi Zanzibar itaendelea kutoa kipaumbele kwa kutenga bajeti ili kuendekeza kazi hii ya urasimishaji ",alisisitiza Rais Dkt. Mwinyi

Akifafanua amesema kuwa mpango wa urasimishaji utasaidia wananchi  wengi zaidi kupata mitaji ya kukuza biashara na shughuli za uzalishaji.

Aidha, Mhe. Rais Mwinyi amesema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar itafanyia kazi mapendekezo yaliyotolewa na Makamu Mwenyekiti wa Mpango huo Bi. Immaculata Senje ikiwemo kuendelea kutenga bajeti ya urasimishaji.

"Mapendekezo yaliyotolewa na Mpango huu ndizo ahadi zangu za uchaguzi kwa wananchi ikiwemo kuweka mazingira wezeshi kwa wajasiriamali wadogo ili waweze kufanya kazi zao kwa tija ",alisisitiza Mhe.Rais   Dkt. Mwinyi

Aliongeza kuwa kujengwa kwa vituo  jumuishi vya biashara vipatavyo 10 visiwani Zanzibar kutasadia kuwawezesha wananchi wengi kurasimisha biashara zao na kuondokana na adha ya urasimu , hii ikiwa ni moja ya ahadi zake wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.

Akizungumzia ahadi zake kwa wananchi Mhe.Rais Dkt. Mwinyi amesema kuwa ni pamoja na; kuwezesha wananchi kupata mitaji ambapo mpango huo unatoa majibu ya changamoto zinazowakabili wananchi katika sekta ya ardhi na biashara kwa kuwaunganisha na Taasisi za fedha kupitia hati zao za kumiliki ardhi.

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ya MKURABITA Bi. Immaculata Senje amempongeza Mhe. Rais Dkt.Hussein Ali Mwinyi na Mhe. Rais Dkt. John Magufuli kwa kuchaguliwa na wananchi kwa kura nyingi.

Aliongeza kuwa MKURABITA imepanga kusajili wajasiriamali 1500, kupima viwanja 5700 katika wilaya za Pemba na Unguja, kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa urasimishaji ardhi na Biashara .

Pia, mpango huo utaendelea kuwaunganisha wananchi na taasisi za fedha ili waweze kukuza mitaji kwa kutumia hati miliki zao za kumiliki ardhi kujikwamua kiuchumi.

Naye Mratibu wa Mpango huo CPA Dkt. Seraphia Mgembe amesema kuwa MKURABITA itaendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuhakikisha kuwa azma ya kujenga uchumi wa buluu inatekelezwa kwa vitendo ili wananchi wafurahie matunda ya urasimishaji.

Aliahidi kuendelea kutoa msukumo katika kuwaelimisha wananchi ili watumie rasilimali ardhi kupata mitaji kupitia hati zao baada ya urasimishaji.

Wajumbe wa Kamati ya Uongozi ya MKURABITA wanahitimisha ziara yao Visiwani Zanzibar Februari 12, 2021, Aidha katika ziara hiyo walishiriki katika ufunguzi wa kituo jumuishi cha Biashara Darajani Zanzibar, kutoa hati miliki za kumiliki ardhi 50 kwa wakazi wa Shehia ya Welezo, kuwatembelea wanufaika wa Mpango huo na kujionea shughuli zao na manufaa waliyopata baada ya urasimishaji.

Ziara ya wajumbe wa Kamati hiyo ilianza Februari 7,2021 na imehitimishwa kwa wajumbe hao kupata fursa ya kukutana na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi .


 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...