Na Beatrice Sanga-MAELEZO
Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imehamisha kwa mujibu wa sheria mali na madeni yote ya Benki ya Biashara ya China (China commercial bank) kwenda NMB Bank PLC kufuatia kukamilika kwa mchakato wa kupata ufumbuzi wa tatizo la benki hiyo uliohusisha BoT, NMB na viongozi wa Benki ya Biashara ya China, baada ya Benki kuu kubaini kuwa benki hiyo ina upungufu wa mtaji kinyume cha matakwa ya sheria hali iliyosababisha hasara kwenye biashara kwa kipindi chote toka kuanza kutoa huduma za kibenki.
Akizungumza katika ukumbi wa mikutano wa BoT Jijini Dar es Salaam Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania Profesa Florens Luoga, amesema mchakato wa kupata ufumbuzi wa tatizo la Benki ya Biashara ya China umekamilika baada ya kutathmini njia mbalimbali ambapo kwa mamlaka iliyopewa chini ya kifungu cha 58(2) (h) cha Sheria ya mabenki na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006, Benki kuu ya Tanzania imeamua mali na madeni yote ya benki hiyo kuchukuliwa na benki nyingine kama njia ya ufumbuzi.
Aidha Profesa Luoga aliongeza kuwa taratibu mbalimbali za kisheria zinaendelea ili kukamilisha uhamishaji wa mali na madeni ambapo hivi karibuni wateja wenye amana na wadau wengine wataanza kupata huduma za kibenki kupitia NMB Bank PLC.
“Kwa sasa, Benki Kuu, NMB Bank PLC na wadau wengine wanaendelea kuandaa taratibu za kisheria za kukamilisha mchakato wa uhamishaji wa mali na madeni ya Benki ya Biashara ya China kwenda NMB Bank PLC. Wateja wenye amana na wadau wengine wa benki hiyo watataarifiwa tarehe ya kuanza kupata huduma za kibenki kupitia NMB Bank PLC. Wateja wenye mikopo wanatakiwa kuendelea kulipa mikopo kulingana na mikataba yao”, amesema Profesa Luoga
Naye, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB Bi Ruth Zaipuni ameishukuru Benki Kuu kwa kuiamini Benk ya NMB na kuahidi kuwa benki hiyo italinda mali na maslahi ya wateja wote wa Benki ya Biashara ya China na maslahi mapana zaidi ya Sekta ya Benki nchini Tanzania kwa kuhakikisha pesa zinakuwa salama na wateja wote wa Benki ya Biashara ya China wataanza kuhudumiwa na Benki ya NMB katika tawi la NMB Bank House na Tawi la ohio
“Sisi tunaishukuru sana BoT kwanza kwa imani kubwa walioonyesha kwa benki ya NMB na kwa dhamana hii kubwa ambayo wametupatia na kutukabidhi mali na madeni ya benki ya biashara ya china ili kulinda maslahi mapana zaidi katika sekta ya benki Tanzania, napenda kuwahakikishia Watanzania na wateja wa benki ya china kwamba fedha zao zitakuwa salama kabisa”, amesema Bi Zaipuni
Gavana wa Benki Kuu (BoT) Prof. Florens Luoga pamoja na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB,Bi Ruth Zaipuna wakikabidhiana nyaraka za uamuzi wa kuhamisha mali na madeni yote ya Benki ya China Commercial Bank Limited kwenda kwa benki ya NMB Bank PLC baada ya kubaini upungufu wa mtaji kinyume na matakwa ya sheria
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...