Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Mheshimiwa Othman Masoud Othman, ameuhimiza uongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar kuzingatia maslahi na thamani ya walimu katika utekelezaji wa majukumu yao kwa lengo la kukuza ubora katika sekta ya elimu nchini.

Mheshimiwa Othman ameyasema hayo katika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi katika ujenzi wa banda la kusomea katika Skuli ya Mtoni Kidatu, Wilaya ya Magharibi 'A' Unguja.

"Tutakapowawekea mazingira bora ya kazi, heshima, mishahara mizuri pamoja na kuthaminiwa katika kupata huduma za kijamii, tutawafanya walimu wetu kuwa na hamasa na kuukuza utendaji wao,”alieleza Makamu wa Kwanza wa Rais.

Mheshimiwa Othman amesema walimu wamekuwa wakipata changamoto mbali mbali katika utekelezaji wa kazi zao, hivyo kuwajengea mazingira wezeshi ya kielimu na hata katika upatikanaji wa huduma za kijamii kutawapa uwezo wa kufanya kazi zao kwa ufanisi.

"Hapo zamani mtu aliyekuwa na heshima kubwa katika kijiji ni mwalimu. Hivyo serikali hatuna budi kuhakikisha tunamrudisha mwalimu kuwa mtu mwenye heshima na hadhi katika jamii,” alifafanua Mheshimiwa Othman.

Aidha ameipongeza Kamati ya Wazee wa Skuli hiyo pamoja na wadau wengine wa elimu kwa juhudi zao kubwa walizozichukua katika kuhakikisha banda hilo linasimama pamoja na kuwaomba kuendelea kushirikiana na Serikali kuongeza nguvu na kuboresha miundombinu mbalimbali ya elimu nchini.

Mbali na hayo, Mheshimiwa Othman ameahidi kuzifanyia kazi changamoto mbali mbali zilizopo katika maeneo hayo kwa lengo la kukuza maendeleo ya wananchi.

Naye Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Mheshimiwa Simai Mohammed Said, alisema wizara bado inaendelea kutafuta fursa mbalimbali katika kuhakikisha matatizo yanayoikumba sekta ya elimu nchini yanamalizika pamoja na kuwaomba wazee kutenga muda wa kuwashughulikia watoto wao katika masomo wanapokuwa majumbani  ili kukuza ufaulu nchini.

Akiwasilisha taarifa ya ujenzi wa banda hilo mjumbe wa kamati ya ujenzi ya skuli hiyo, Bwana. Juma Shaame Khamis, ameiomba Serikali kuwasaidia kumalizia hatua iliyobakia ikiwemo utiaji wa plasta, sakafu  na madirisha.

Mbali na hilo, Kamati hiyo imeiomba serikali kuwajengea jengo jengine litakalowasaidia wanafunzi wa Sekondari ambao kwa sasa wanalazimika kutumia madarasa ya wanafunzi wa Msingi kutokana na tatizo la uhaba wa madarasa linaloikabili skuli hiyo.

Takriban shilingi milioni ishirini na tatu zimetumika katika ujenzi wa banda hilo lenye madarasa sita na ofisi mbili za walimu.


Kitengo cha Habari
Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...