NA KHALFAN SAID, SABASABA
WANACHAMA wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) wameaswa kuwa na utaratibu wa kujua taarifa na mwenendo wa michango yao mara kwa mara tangu siku walipoajiriwa, Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Mfuko huo Bw. Mbaruku Magawa amesema.
Bw. Magawa ameyasema hayo leo Julai 7, 2021 alipokuwa akitoa tathmini yake ya huduma zinazoendelea kutolewa na Mfuko kwa wanachama, wastaafu na wanaanchi kwa ujumla kwenye maonesho ya 45 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanayoendelea kwenye viwanja vya Julius Nyerere maarufu Sabasaba jijini Dar es Salaam ambapo PSSSF iko kwenye banda namba 13 la Ushirikiano linalotumiwa pia na NSSF.
“Wanachama wasisubiri kustaafu ndipo waje waanze kufahamu maswala yao, kuanzia ile siku ya kwanza mwanachama anapoajiriwa au mtumishi sasa huyo, angalau kila mwaka unapaswa kujua hivi maswala yangu ya kustaafu yatakuwaje hilo ni suala muhimu sana, na unapoanza kuwaza kustaafu basi unaiwaza PSSSF.” Alisema.
Akifafanua zaidi alisema wanachama wa PSSSF ni watumishi wote wa umma ambao kwa mujibu wa sheria ni kila taasisi ambazo serikali angalau ina hisa zinazozidi asilimia 30%.
Alisema baada ya kuandiskishwa mwanachama ataanza kuchangia na hapo ndipo anapaswa kuanza kujua taarifa zake.
“Sasa hivi tumerahisisha sio lazima uende kwenye ofisi za mfuko ili kujua taarifa zako, unaweza ukiwa ofisini kama unatumia computer, unaweza kuingia kwenye website yetu na ukajua taarifa zako za michango zinakwendaje, na hata majukumu ya kiofisi yanapokuzidi unaweza kwa muda wako ukatumia simu yako ya kiganjani na ukapata taarifa.” Alifafanua Bw. Magawa. Na kuongeza……umuhimu wa kujua taarifa zako, itakuwezesha kujua mwendendo wa michango yako ikiwa ni pamoja na kujua mosi michango inayokwenda kwenye mfuko inaenda kulingana na mshahara unaoupata mwanachama, lakini pia kujua kama michango yako inakwenda, hayo ni mambo muhimu sana.”
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...