NA BALTAZAR MASHAKA, Mwanza
MWENYEKITI wa Taasisi ya Mzalendo Foundation,Khamis Mgeja amewafananisha na magaidi watu wanaopotosha kuhusu chanjo ya kuzuia maambukizi ya Virusi vya Homa Kali ya Mapafu (UVIKO-19) na kuiomba serikali kuwachukulia hatua za kisheria.
Mgeja ambaye ni Mwenyekiti wa CCM mstaafu wa CCM Mkoa wa Shinyanga, alitoa ombi hilo wakati akihojiwa kwa njia ya simu jana baada ya kupata chanjo ya Uviko 19.
Alisema wapotoshaji wa chanjo ya Uviko-19 ni sawa na magaidina upotoshaji huo ni aina mpya ya ugaidi hivyo serikali isiwafumbie macho badala yake iwachukulie sawa na wahalifu wengine.
“Kama unazuia watu wasichanjwe maana yake unataka wafe, kwa hiyo hawa ni sawa na magaidi,wanaopotoshaji hao dhidi ya chanjo ya Uviko-19 wachukuliwe sawa na wahalifu wengine, hao ni sawa na wauaji wa Kimbari hivyo wachukuliwe hatua za kisheria, tusiwachekee kwani ukicheka na nyani utavuna mabua,"alisema Mgeja.
Mwenyekiti huyo wa Mzalendo Foundation alisema kuwa taaluma ya kitaalamu inakosolewa kitaalamu siyo kuingiza siasa na upotoshaji, watu hao wanaopinga chanjo ya Uviko-19 ni bora wakae kimya au watupe mbadala wa chanjo hiyo kuliko kuwapotosha watu.
"Ninampongeza Mhe. Rais Samia Suluhu kwa kukubali Watanzania wapatiwe chanjo dhidi ya Uviko-19, binafsi nimejitokeza kuwa miongoni mwa Watanzania wa mwanzo kabisa kuchanjwa chanjo hii dhidi ya Uviko-19,”alisema Mgeja na kuwaomba wananchi wengine wajitokeze kuchanjwa.
“Akili za kuambiwa changanya na za kwako, wapuuzeni hao wapotoshaji ni magaidi jitokezeni mkachanjwe chanjo hii ni salama kwa mujibu wa wataalamu,lakini pia nampongeza Mkuu wetu wa Mkoa wa Shinyanga Dk. Philemon Sengati kwa namna alivyowahamasisha wananchi ili wapate chanjo,” alieleza.
Mwenyekiti wa Taasisi ya Mzalendo Foundation na Mwenyekiti mstaafu wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Khamis Mgeja akipata chanjo dhidi ya Uviko-19 jana baada ya chanjo hiyo kuzinduliwa na Mkuu wa Mkoa huo, Dk. Philemon Sengati. Picha na Baltazar Mashaka
Mwenyekiti wa Taasisi ya Mzalendo Foundation, Khamis Mgeja akizungumza muda mfupi baada ya kupata chanjo dhidi ya Uviko- 19 jana.Picha na Baltazar Mashaka
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...