Na Mwandishi Wetu,Michuzi Blog
WADAU mbalimbali nchini wameombwa kujitokeza kwa wingi katika maonesho ya wiki ya AZAKI inayotarajiwa kuanza Oktoba 23 mwaka huu katika Jiji la Dodoma.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Oktoba 18,2021 katika Ofisi za Foundations For Civil Society (FCS) mkoani Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Legal Services Facility Tanzania (LSF), Lulu Ng'wanakilala amesema kwamba mgeni rasmi katika naonesho ya Wiki ya AZAKI anatarajiwa kuwa Spika wa Bunge Job Ndugai.
Amesema Spika Ndugai ni kingozi anayesimamia muhimili wa Bunge ambao ni moja ya mihimili ya nchi, hivyo pamoja na mambo mengine atapata fursa ya kuona kazi zinazofanywa na asasi za kiraia ambapo kauli mbiu ya maonesho hayo mwaka huu ni ''Azaki na Maendeleo"
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi ya TANGO Ramadhan Masele amesema katika siku saba za maonesho hayo kutakuwa na matukio mbalimbali yatakayokuwa yanafanyika katika Jiji la Dodoma.
Ameongeza kuwa moja ya mambo ambayo yatafanyika ni utoaji wa msaada wa kisheria kwenye Mabanda mbalimbali lakini pia kutakuwa na utolewaji wa elimu kuhusu chanjo ya Uviko - 19.
Pia Oktoba 24 mwaka huu kutakuwa na mijadala mbalmbali ikiwano kuangalia namna ambavyo wanashirikiana na Serikali na mengine mengi yanayohusu maendeleo ya nchi kwa ujumla.
Wakati huo huo Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria LHRC Anna Henga amesema katika maonesho hayo kutakuwa na utoaji wa tuzo mbalimbali ikiwa ni eneo la jinsia, uwajibikaji kwa Jamii, walemavu, na mengineyo ambapo tuzo hizo zitatolewa na Waziri wa Afya,Maendeleo ua Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto Dk.Dorothy Gwajima Ocktoba 28,2021.
"Kuna asasi nyingi zinazofanya kazi vizuri hivyo tutatambua mchango wao katika maendeleo ya nchi kupitia wiki hiyo ya Azaki,tutaendelea kushirikiana na sekta binafsi kwenye nyanja mbalimbali.Tunawaomba wadau na wananchi kujitokeza kwa wingi katika maonesho hayo.
Kwa upande wa Mkurugenzi Mtendaji wa FCS Francis Kiwanga amesema wao kama Azaki wanatambulika na Serikali, wanapata ushirikiano mkubwa na chini ya Rais Samia Suluhu Hassan ambaye ametoa muelekeo mzuri.
Amesema maonesho hayo wanatarajia kujadili maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa kwao na hivyo sehemu ya maonesho hayo itakuwa na majadiliano.
Ameongeza katika maonesho hayo wamejipanga kuhakikisha wananchi wanapata faida kupitia wiki hiyo na katika hilo wanatambua umuhimu wa waandishi wa habari na ndio maana wamekuwa nao nyakati zote.
"Lengo letu kubwa nikuona kila kinachofanyika wananchi wanakipata na kinawafikia hivyo kutakuwa na jopo la waandishi wa habari kutoka Dar es salaam na wengine watakuwa wa Dodoma,"amesema Kiwanga.
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Legal Services Facility Tanzania (LSF) Lulu Ng'wanakilala (wa pili kushoto) akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maonesho ya wiki ya Azaki yanayojarajiwa kuanzia Oktoba 23,mwaka huu jijini Dodoma, (wa kwanza kushoto) ni Mkurugenzi wa Taasisi ya TANGO Ramadhan Masel, (wa tatu kushoto) ni Anna Henga Mkurugenzi wa kituo cha sheria LHRC, na (wa kwanza kulia) ni Mkurugenzi Mtendaji wa FCS Francis Kiwanga
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Legal Services Facility Tanzania (LSF) Lulu Ng'wanakilala akizungumza na waandishi wa habari (hawamo pichani) wakati wa mkutano wao kuzungumzia Wiki ya Azaki 2021 Jijini Dodoma.
Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binaadam (LHRC) Anna Henga akizungumzia tuzo mbalimbali zitakazotolewa na Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto Dk. Dorothy Gwajima Ocktoba 28,2021.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...