Shirika la Reli Tanzania laendelea na Wiki ya TRC kwa kufanya ziara jijini Mwanza katika vyombo vya habari nchini ambako reli imepita, Februari 2022.

Lengo la Wiki ya TRC ni kuuhabarisha umma kuhusu shughuli mbalimbali za Shirika ikiwemo huduma za usafiri wa abiria na usafirishaji mizigo, masuala ya usalama wa reli halikadhalika Miradi ya kimkakati inayosimamiwa na Shirika ikiwemo mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa – SGR ambao unaendelea kwa wamau ya kwanza Dar es Salaam – Mwanza katika vipande vya Dar es Salaam – Morogoro, Morogoro – Makutupora, Isaka – Mwanza na Makutupora – Tabora ambacho mkataba wake umesainiwa hivi karibuni Disemba 2021.

Akiwa katika Shirika la Utangazaji Nchini – TBC Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania alieleza kuwa “Tuko kwenye Wiki ya TRC na lengo kubwa ni kuwahabarisha watanzania kuhusu nini tunafanya, uendeshaji wa treni na ujenzi wa miundombinu, tulifanya mkutano na waandishi wa habari na sasa tunaendelea na ziara kwenye vyombo vya habari”

Wiki ya TRC huadhimishwa na Shirika kila mwaka ambapo kitengo cha Habari na Uhusiano kwa kushirikiana na Idara nyingine za Shirika huandaa ziara katika vyombo vya Habari katika mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro, Dodoma, Singida, Tabora, Shinyanga, Simiyu, Mwanza, Tanga, Kilimanjaro na Arusha.

“Hii reli imepita mikoa 16, kwahiyo wananchi ndio walinzi wa kwanza wa reli ukizingatia kwamba zimetumika zaidi ya trilioni 14.7 kwenye mradi wa SGR ambazo ni pesa za wananchi hivyo tunawaelimisha katika Wiki hii ya TRC ili wajue kuwa reli hii ni mali yao” alisema Kadogosa

Akizungumza kuhusu majaribio ya treni za kisasa za SGR Ndugu Kadogosa alieleza kuwa majaribio ya njia pamoja na mifumo mingine ya reli ya kisasa yalianza mwezi Oktoba 2021 na yanaendelea, kilichobaki ni majaribio kwa kutumia treni ambazo zinatarajiwa kuwasili nchini Aprili 2022.

“Majaribio tumeanza tangu Oktoba 2021, tunafanya majaribio ya njia, madaraja na mifumo ya umeme na hatua ya mwisho itakuwa ni kupitisha treni ambayo itafanya majaribio ya mifumo yote, majaribio hayo yataanza mara baada ya treni kuwasili mwishoni mwa mwezi Aprili 2022” alisema Kadogosa

Kadogosa aliongeza kuwa “Mkandarasi naye anaendelea na majaribio kwa kutumia treni yake inayotumia Dizeli lakini tarehe 17 Februari 2022 ataleta kichwa kinachotumia umeme na ataanza majaribio ya umeme”

Mkurugenzi Mkuu katika ziara yake katika vyombo vya Habari mkoani Dar es Salaam alieleza baadhi ya faida na sababu za utekelezaji wa mradi wa reli ya kisasa kuwa ni kuunganisha ukanda wa Afrika Mashariki pamoja na Afrika kwa ujumla kwakuwa mradi huu uliwekwa kwa makubaliano baina ya nchi za Afrika kwa lengo la kurahisisha shughuli za kijamii na kiuchumi.

“Reli ina historia kubwa katika taifa, ni zaidi ya miaka 100, mjerumani alijenga, akaja muingereza akajenga kidogo lakini baada ya uhuru Hayati Mwalimu Nyerere alijenga, hivi sasa tunazungumzia reli ya kisasa (standard gauge), hii ni kwamba unaweza ukaenda, Kigali, Bujumbura, Uganda na ukarudi hii ndiyo maana ya ‘Standard’ kwa maana ni reli yenye viwango vinavyotumika karibu Dunia nzima” aliongeza Kadogosa.

Mkurugenzi Mkuu TRC ameeleza kuwa mradi wa SGR unaendelea vizuri ambapo kwa kipande cha Dar es Salaam – Morogoro (km 300) kimefika 95%, kipande cha Morogoro – Makutupora (km 422) kimefika 81%, kipande cha Isaka – Mwanza (km 361) kimefika 4% huku kipande cha Makutupora – Tabora (km 361) kipo katika hatua za awali za maandalizi kwa ajili ya kuweka jiwe la msingi na kuanza ujenzi. 

Kwa upande wa behewa na vichwa vya treni Kadogosa amesema kuwa Serikali imeagiza behewa za kubeba abiria, treni zenye vichwa mbele na nyuma (EMU) ambazo mara nyingi zinakwenda masafa mafupi, behewa za kawaida ambazo zitakuwa kwa ajili ya masafa marefu ambazo ziko 59, vichwa 17, pia Serikali imeagiza behewa 30 za gorofa na vichwa viwili vya treni ambavyo vitaanza kwa ajili ya majaribio.

Aidha, Kadogosa amemshukuru Mhe. Rais Samia kwa maamuzi haya, ndani ya muda mfupi ameweza kufanya mambo makubwa, kipindi anapokea uongozi tulikuwa tunajenga vipande viwili lakini mara baada ya kuanza uongozi wake tumeona tayari vipande viwili vimeshatiliwa saini kwa ajili ya ujenzi.

Wiki ya TRC inaendelea ambapo hivi sasa timu ya mawasiliano ikiongozwa na Mkurugenzi Mkuu Masanja Kadogosa iko Mwanza na baadaye itaendelea na ziara hiyo katika mikoa ya Simiyu, Shinyanga, Tabora, Singida, Dodoma, Morogoro na kuhitimisha katika mikoa ya Tanga, Kilimanjaro na Arusha.

Shirika linawaomba wananchi kufuatilia Wiki hii katika vyombo vya Habari pamoja na mitandao ya kijamii ili waweze kupata taarifa na elimu sahihi kuhusu shughuli zinazofanywa na shirika sambamba na masuala ya usalama wa reli ili miundombinu ya reli iendelee kuwa salama kwa matumizi ya sasa na kwa vizazi vijavyo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...