Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA,) Bi. Consolatha Mushi akizungumza na waandishi wa habari wakati akitoa mkakati wa utekelezaji wa  maelekezo yaliyotolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzanaia Dkt. Philip Mpango juu ya kuanza kwa utekelezaji wa matumizi ya lugha ya Kiswahili ili kuendana na maendeleo yake ya kasi ulimwenguni.



* Serikali yatoa maagizo utekelezaji yaliyotolewa na Makamu wa Rais ili kuendana na kasi ya maendeleo ya lugha ya Kiswahili duniani

LUGHA ya Kiswahili imeendelea kutandawaa ulimwenguni kote baada ya toleo jipya la kamusi ya lugha ya kiingereza ya Oxford  kuingiza maneno ya Kiswahili takribani mia mbili tofauti na mwaka juzi ambapo kamusi hiyo iliingizwa maneno ya Kiswahili matano pekee.

Hayo yameelezwa leo na Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA,) Bi. Consolatha Mushi wakati akitoa mkakati wa utekelezaji wa  maelekezo yaliyotolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzanaia Dkt. Philip Mpango katika siku ya maadhimisho ya siku ya Kiswahili ulimwenguni iliyofanyika Julai saba mwaka huu na kuelekeza kuanza rasmi kwa utekelezaji wa matumizi ya lugha ya Kiswahili ili kuendana na maendeleo yake ya kasi ulimwenguni.

''Tunafahamu kamusi ya Oxford inatumika sana duniani, ni kamusi ya kiingereza ila katika toleo hili imehusisha maneno ya Kiswahili mengi zaidi, hii ni tabia ya lugha ya kuchota maneno katika lugha nyingine, na inatupa fahari kubwa na inadhihirisha kuwa Kiswahili kimefika mbali.'' Amesema.

Amesema baadhi ya maneno yaliyoingizwa katika kamusi hiyo ni pamoja na neno 'daladala' likimaanisha magari yanayotumika kusafirisha abiria na 'jembe' kifaa kinachotumika kulimia.

''Maneno yaliyoingizwa katika kamusi hii na kuwa rasmi ni maneno yaliyozoeleka kimatumizi, neno 'chapo' likimaanisha chapati linalotumika sana nchini Kenya limeingizwa katika kamusi hiyo, pia neno 'Mama Ntilie ' limeingizwa katika kamusi ya Oxford kwa maana ya Mama anayepika chakula na kuwauzia watu kwa gharama nafuu ili kila mtu aweze kumudu na kupata chakula, aidha neno 'Singeli' limechukuliwa kama muziki ambao asili yake ni Tanzania, neno 'Kolabo' na 'sambaza' pia yameingizwa katika Oxford...Hii ni dhahiri kuwa Kiswahili kwa sasa kinaenda kwa kasi kubwa.'' Amesema.

Aidha amesema kuwa, Kiswahili kinazungumzwa na watu wapatao milioni 500 duniani msamiati wake unakua na kukuza lugha nyingine na kuingizwa kwa maneno hayo katika kamusi ya Oxford kutasaidia katika kusambaza msamiati wa Kiswahili pamoja na utamaduni wa Mswahili.

''Neno jingine lililoingizwa katika kamusi ya Oxford ni 'chips yai', wengi watataka  kufahamu chakula hiki cha chips yai kipoje na kinatengenezwaje tayari tumepeleka utamaduni wa vyakula katika lugha ya kiingereza..Hii ni tija kubwa na fahari kubwa mabaraza yapo kwa ajili ya kutengeneza msamiati ili kusonga mbele zaidi.'' Ameeleza.

Amesema kuwa mabaraza yaliyoundwa kisheria yataendelea kufanya usanifishaji na utafiti mkubwa wa kuchukua maneno mengine ya lugha za kiafrika na kuyaingiza katika lugha ya Kiswahili.

Akitoa tamko juu  hatua ya kuanza utekelezaji wa maagizo ya matumizi ya lugha ya Kiswahili ili kuendana na kasi ya maendeleo ya lugha ya Kiswahili yaliyotolewa na Makamu wa Rais Dk. Philiph Mpango, kwa niaba ya Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mohamed Mchengerwa  Bi. Consolatha amesema kuwa maagizo hayo yanayotakiwa kuanza kutekelezwa kuanzia sasa ni pamoja na nyaraka za Serikali kati ya ofisi moja na nyingine, idara na idara, taasisi za Umma na binafsi na mashirika kuandikwa kwa lugha ya Kiswahili na ikiwa nyaraka hizo zinaandikwa kwa mgeni nyaraka mbili za kiingereza na Kiswahili zitumike.

''Makamu wa Rais pia ameelekeza katika majina ya barabara, mitaa na majina ya vifaa mbalimbali yaandikwe kwa lugha ya Kiswahili..Katika zoezi linaloendelea nchini la kuweka majina ya mitaa tumeona lugha inayotumika pengine inakosewa hivyo agizo la Makamu wa Rais la kuandika majina ya mitaa kwa lugha ya Kiswahili lizingatiwe na lugha itakayoandikwa iwe fasaha na sanifu..Baraza lipo tayari kutoa msaada wa kuhakiki majina hayo.'' Amesema.

Aidha amesema maeneo mengine ambayo utekelezaji wake unapaswa kuanza mara moja ni pamoja na mabango ya matangazo yote yaliyopo barabarani kuwa katika lugha ya Kiswahili, maelezo ya bidhaa zote zinazozalishwa viwandani,fomu za usahili pamoja maelezo ya matumizi ya dawa yawe kwa lugha ya Kiswahili ili kuweza kumlinda mlaji dhidi ya athari hasi zinazoweza kutokea kwa kushindwa kuelewa maelezo yaliyotolewa.

''Miradi yote inayohusu wananchi lazima iandikwe kwa Kiswahili ili kuwasaidia wananchi kuelewa miradi hiyo, sheria na kanuni zinaendelea kutafsiriwa kwa Wizara ya Katiba na Sheria kwa kushirikiana na Baraza ili kukipeleka Kiswahili mbele zaidi..BAKITA na BAKIZA tunaendelea kusimamia utekelezaji wa maelekezo ya maagizo hayo.'' Amesema.

Aidha amevitaka vyombo vya habari vinavyotumia lugha ya Kiswahili kuzingatia agizo la Makamu wa Rais la kuzingatia matumizi sahihi na fasaha na sanifu ya Kiswahili na wakishindwa watumie mabaraza ya kuelekezwa matumizi fasaha ya lugha.


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...