Na Bakari Madjeshi, Michuzi TV
Azam FC wamepata ushindi wa bao 1-0 katika mchezo wa mzunguko wa 15 wa Ligi Kuu Soka Tanzania Bara (NBC PL) msimu wa 2022-23 dhidi ya Polisi Tanzania FC kwenye uwanja wa Ushirika mjini Moshi mkoani Kilimanjaro.
Azam FC ilipata bao lake la ushindi katika dakika ya 15’ kipindi cha kwanza kupitia kwa Mshambuliaji wake Ayoub Reuben Lyanga aliyeunganisha ‘krosi’ ya Pascal Msindo iliyotoka upande wa kushoto.
Polisi Tanzania FC imepoteza mchezo huo ikiwa ni siku chache tangu kumtangaza Kocha wa zamani wa Yanga SC, Mwinyi Zahera kuwa Kocha Mkuu wa Kikosi hicho cha Maafande wa Jeshi la Polisi.
Hata hivyo, hali si shwari kwa Polisi Tanzania FC ambao hadi sasa kwenye msimamo wa Ligi Kuu wanaburuza mkia wakiwa na alama 9 pekee na tayari wamemaliza michezo 15 ya mzunguko wa kwanza wa Ligi hiyo, wamebakiwa na michezo 15 ya mzunguko wa pili ili kumaliza Ligi salama bila kushuka daraja.
Vijana wa Chamazi, Azam FC baada ya ushindi huo wamepanda hadi nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu wakiwa na alama 35 sawa na Yanga SC wenye alama kama hizo tofauti ikiwa ni michezo iliyochezwa kwenye mzunguko wa michezo 15 ya Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu.
Yanga SC nafasi ya kwanza kileleni mwa msimamo wakiwa na alama hizo 35 wakiwa na faida ya mchezo mmoja wa kiporo, huku Azam FC nafasi ya pili wakiwa na michezo 15.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...