Na. Saidina Msangi, WFM, Dodoma
SERIKALI imesema kuwa imeanzisha kitengo maalum kinachosimamia biashara za mtandao, ikiwa ni pamoja na kubuni na kuboresha mifumo ya usimamizi wa biashara za mtandao ili kuwezesha utambuzi, usajili na ukusanyaji wa kodi stahiki.
Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Hamad Hassan Chande (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mheshimiwa Judith Salvio Kapinga, aliyetaka kujua kuhusu mkakati wa Serikali wa kuimarisha ukusanyaji mapato katika biashara zinazofanyika mtandaoni.
Mheshimiwa Chande alisema katika kuimarisha ukusanyaji wa mapato, Serikali kupitia Sheria ya Fedha ya mwaka 2022, ilifanya marekebisho ya Sheria ya Kodi ya Mapato, SURA 332 na Sheria ya Ongezeko la Thamani, SURA 148 ili kuwezesha kutoza kodi kwenye biashara zinazofanyika kwa njia ya mtandao.
‘’Mamlaka ya Mapato Tanzania, imeanzisha kitengo maalum kinachosimamia biashara za mtandao, ikiwa ni pamoja na kubuni na kuboresha mifumo ya usimamizi wa biashara za mtandao ili kuwezesha utambuzi, usajili na ukusanyaji wa kodi stahiki’’, alisema Mhe. Chande.
Alifafanua kuwa mikakati mingine ni pamoja na kuwajengea uwezo maafisa kodi juu ya namna ya kutathmini na kukusanya mapato ya kodi yanayotokana na biashara za mtandaoni.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Hamad Hassan Chande (Mb) alikijibu swali, bungeni jijini Dodoma.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...