Na Chalila Kibuda, Michuzi TV
Kamati ya kudumu ya bunge ya TAMISEMI imeridhishwa na kasi ya utekelezaji wa ujenzi wa miundombinu ya mfumo wa usafiri mabasi Yaendayo Haraka (BRT) Dar es Salaam awamu ya tatu kutoka Gerezani hadi Gongolamboto.
Kamati hiyo imeitaka DART kuongeza idadi ya mabasi ili biashara ya usafiri iwe yenye ufanisi katika kutoa huduma bora na kufikia malengo yanayotarajiwa na serikali.
Akizungumza katika ziara ya kamati hiyo Makamu Mwenyekiti Kamati ya kudumu ya bunge ya TAMISEMI Justin Nyamoga, amesema kuwa wakati umefika wa BRT kuanza kutumia teknolojia kwa kutumia smart Card jambo ambalo ni rafiki kwa abiria katika kutatua changamoto wakati wa kusafiri na mabasi hayo.
Nyamonga amesema kuwa mifumo ya kisasa ya ukusanyaji wa mapato ni muhimu ili kuleta tija katika utendaji pamoja na kufikia malengo husika.
“Tunawapongeza kwa kutumia wataalamu wa ndani pamoja na kuhakikisha mnaendelea kulinda mifumo, uendelee kuwa wazalendo katika utendaji kazi” amesema Mhe. Nyamonga.
Hata hivyo amesema kuwa serikali inapaswa kutenga maeneo katika miji inayokua kwa ajili ya kuendeleza miradi ili kuepuka kulipa watu fidia wakati wa uendelezaji miradi mbalimbali.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART) Dkt. Edwin Mhede, amesema kuwa kamati ya kudumu ya bunge ya TAMISEMI wametembelea mradi wa awamu ya tatu wa BRT ambao unatoka katikati ya mji kwenda Gonglamboto.
Dkt. Mhede amesema kuwa mpaka sasa utekelezaji ujenzi wa miundombinu ya mfumo wa usafiri haraka wa mabasi (BRT) umefikia asilimia 17.65 ya ujenzi wote.
Dkt. Mhede kuwa mradi huo unatarajiwa kukamilika machi 2024 huku akieleza kuwa mafundi wanaendelea na ujenzi usiku na mchana ili kuhakikisha unakamilika kwa wakati.
“Pia wabunge wamaona changamoto mbalimbali katika utekelezaji wa maradi huu ikiwemo vumbi ambalo linakwenda katika makazi ya watu wakati wa uekelezaji wa mradi huu, na tayari wataalamu wameanza kudhibiti ili kuepuka madhara” amesema Dkt. Mhede.
Dkt. Mhede amesema kuwa wanaendelea kujipanga ili kasi ya ujenzi wa miundombinu iendane na idadi ya mabasi yaendayo jambo ambalo litasaidia kuleta tija na kufikia malengo tarajiwa.
Aidha amesema kuwa anashukuru wananchi kuendelea kutumia usafiri huku mamlaka ikijipanga kuingiza mabasi kwa ajili kutoa huduma hiyo kwa ufanisi.
Mtendaji Mkuu wa DART Dkt.Edwin Mhede akizungumza mara baada ya Kamati ya Bunge ya Kudumu ya TAMISEMI kutembelelea mradi wa ujenzi mradi wa BRT Gerezani hadi Gongolamboto , jijini Dar es Salaam.Baadhi ya mafundi wakiendelea na ujenzi wa mradi wa awamu ya tatu wa ujenzi wa miundombinu ya mfumo wa usafiri wa mabasi yaendayo haraka (BRT) kutoka katikati ya mji hadi Gongo la Mboto.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART) Dkt. Edwin Mhede (wa pili kutoka kulia) akitoa ufafanuzi kwa Makamu Mwenyekiti Kamati ya kudumu ya bunge ya TAMISEMI Mhe. Justin Nyamoga (wa kwanza kushoto) wakati Kamati ya Kuduma ya Bunge ya TAMISEMI wakikagua mradi wa awamu ya tatu wa ujenzi wa miundombinu ya mfumo wa usafiri wa mabasi yaendayo haraka (BRT) kutoka katikati ya mji hadi Gongo la Mboto
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART) Dkt. Edwin Mhede akifafanua jambo kwa kamati ya Kudumu ya Bunge ya TAMISEMI.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...