ZANZIBAR

MKURUGENZI wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA-ZNZ), Dkt. Mzuri Issa, amewashauri wanawake na Vijana kujiamini na kuondosha woga wakati wa kugombea nafasi za Uongozi ili kuleta mabadiliko chanya katika jamii.

Dkt. Mzuri ameyasema hayo akifungua mafunzo ya siku mbili ya uongozi kwa vijana wa kike, yenye lengo la kuwajengea uwezo wa kuungana pamoja na kuleta ushawishi katika maendeleo ya agenda mbalimbali za kitaifa.

Amesema kwa sasa dunia imetambua umuhimu wa mwanamke na imeamini kwamba mwanamke ni Kiongozi kutokana na maendelo tofauti yaliyoletwa na viongozi wanawake duniani.

“Mwanamke ni kiongozi bora, na nyinyi vijana ndio tunawategemea muwe na maono ya mbali katika kuleta uongozi ulio imara na kuibeba nafasi ya mwanamke katika uongozi, mwanamke anaweza kuwa mama, mke, mfanyakazi na kiongozi na wakati huohuo na akaweza kutekeleza majukumu yote hayo na akafanya vizuri katika kila sekta”, Dkt. Mzuri Issa , Mkurugenzi TAMWA ZNZ.

Akitoa mafunzo hayo kwa vijana wa kike 15, Mkufunzi wa masuala ya Uongozi, Imelda Lulu Urrio amesema lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo kujitambua na kutambua nafasi zao ili kufikia ndoto zao katika harakati za Uongozi.

“Nafasi ya wanawake kwa sasa inazidi kuongezeka kwa sababu kuna ukuwaji wa Elimu kwa jamii na hata watoto wa kike wenyewe wameanza kujitambua na kujielewa, tumeona baadhi ya jamii inavyowajenga watoto wa kike kujitambua na kupelekea ongezeko kubwa la viongozi wanawake”, alisema mkufunzi huyo.

Nae Maryam Ame, mratibu wa mradi wa kuwawezesha wanawake kushika nafasi za Uongozi (SWIL) unaotekelezwa na TAMWA ZNZ kwa kushirikiana na Ubalozi wa Norway amesema mda mrefu imeonekana wanawake wameachwa nyuma katika ngazi za maamuzi hivyo kwa sasa wanawake watumie fursa na haki yao ya kikatiba ya kuchagua na kuchaguliwa ili kufikia dhamira ya 50/50 katika masuala ya uongozi.

Aidha washiriki wa mafunzo hayo wamesema wamefarijika kupata mafunzo hayo kwani yanawajenga kuwa viongozi bora na kuahidi kuwatakuwa mabalozi wazuri kwa wanawake na kupambana kugombania nafasi za ngazi za juu ili kuondosha mfumo dume uliotawala katika jamii.

“Matarajio yangu baada ya mafunzo haya ni kuwa Kiongozi mwenye kujiamini, na nitapambana kuwa kiongozi wa ngazi za juu zaidi katika chuo changu,” alieleza Hudhaimat Haji Juma, mwanafunzi wa Shahada ya Pili ya Uhasibu katika Chuo Kikuu cha Taifa, (SUZA).

Mafunzo hayo yameendeshwa ikiwa ni mwendelezo wa utekelezaji wa mradi wa kuwawezesha wanawake kushika nafasi za uongozi (SWIL), unaotekelezwa kwa pamoja na TAMWA ZNZ, PEGAO NA ZAFELA kwa mashirikiano na Ubalozi wa Norway.
Mkurugenzi TAMWA ZNZ, Dkt. Mzuri Issa akizungumza wakati wa mafunzo ya uongozi kwa Vijana wa kike.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...