NA
K-VIS BLOG, MBEYA
MFUKO
wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umeendelea na kampeni yake ya
kuwapatia miche ya miti wastaafu watarajiwa wa Mfuko huo katika semina
zinazoendelea kwenye mikoa mbalimbali nchini za maandalizi ya kustaafu utumishi
wa umma kwa wastaafu watarajiwa wa Mfuko huo.
Septemba
19, 2023 ilikuwa ni zamu ya wastaafu watarajiwa wa mkoa wa Mbeya waliopatiwa
miche hiyo sanjari na elimu ya maandalizi ya kustaafu utumishi wa umma kwenye
ukumbi wa Mkapa jijini humo. Mgeni rasmi alikuwa ni Mkuu wa Mkoa Mhe. Juma
Homera.
Viongozi
wa PSSSF wakiongozwa na Mkurugenzi wa Uwekezaji, Bw. Fortunatus Magambo na
Mkurugenzi wa Ununuzi na Ugavi Bw. Ernest Khisombi kwa niaba ya Mkuurgenzi Mkuu
CPA. Hosea Kashimba, waligawa miche kwa wastaafu watarajiwa ikiwa ni mpango wa
PSSSF kuunga mkono juhudi za serikali za kukabiliana na mabadiliko ya
Tabianchi.
Wakati
akizindua kampeni hiyo Septemba 11, 2023 jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu
wa PSSSF, CPA. Hosea Kashimba alisema “Tumekuja na kampeni ya upandaji miti kwa
hisani ya Mfuko wa PSSSF, tunaomba mtusaidie mtakaporudi maofisini muwaeleze
wenzetu ambao ni miongoni mwa wanachama wa PSSSF, kila mfanyakazi atupandie mti
mmoja uitwe PSSSF, hii itasaidia kuwa na mchango mkubwa kwa taifa letu,
hatuwezi kuwa na hifadhi ya jamii huku jua likiwaka linawaka kweli kweli,
linaathiri ustawi wetu, au upepo ukivuma unang’oa mabati yetu. Ni muhimu
tutengeneza mazingira yetu yatakayotufanya tuishi mahali salama sisi na vizazi
vijavyo.”
Hapa
jijini Mbeya Mkurugenzi wa Uwekezaji PSSSF, Bw. Fortunatus Magambo, ambaye
alimuwakilisha CPA. Kashimba alisema kupitia mpango huo, PSSSF inakusudia
kuwapatia miche ya miti, wanachama wake wapatao 739,000 nchi nzima wakiwemo
watumishi wa Mfuko huo.
“Pia
kwa kushirikiana na watumishi wa Mfuko tutaendesha kampeni ya kuhakikisha kila mtumishi
anapanda na kuitunza miche kumi ya miti, kampeni hii itaendelea hadi Disemba
2023 ambako tunatarajia tutakuwa tumepanda miche takribani million 7.” Alisema
Akizungumzia
kuhusu semina hiyo Bw. Magambo alisema, PSSSF inatarajia kuwa na wastaafu 11,000
katika kipindi cha mwaka wa fedha 2023/2024.
Alisema Wastaafu watapatiwa mafunzo ya elimu ya uwekezaji katika masoko ya fedha, taarifa za nyaraka na utaratibu wa kufuata wakati wa kustaafu, kujiandaa kisaikolojia baada ya kutoka kwenye utumishi, umuhimu wa kutunza mazingira tunayoishi kutokana na mabadiliko ya Tabianchi, na uhalifu wa kimtandao ambao unawaathiri wastaafu wengi.
Katika
nasaha zake kwa wastaafu hao watarajiwa wa PSSSF, mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa
Mbeya, Mhe. Juma Homera amesema, semina hizi matokeo yake yatakuwa mazuri iwapo
tu wastaafu hao watarajiwa watazingatia mafunzo waliyopewa.
“Kama
serikali na kama mwajiri mategemeo yetu ni kuona matokeo chanya kupitia kwenu,
na mimi niseme wazi kwamba nitaanza kuwafatilia ili nione nini mnakifanya kwa
maendeleo yenu, mkoa wetu na taifa letu kwa ujumla.” Alisema Mhe. Homera.
Aliwahimiza
washiriki hao kuwa na namna bora na sahihi ya kutumia fedha wanazolipwa baada
ya kustaafu, na ameonyesha imani yake kuwa mafunzo hayo yatakuwa suluhisho la
wastaafu kutapeliwa fedha za mafao na wajanja wachache.
Ni
matumaini yangu baada ya mafunzo hayo mtapata uelewa juu ya matumizi sahihi ya
fedha na kuwekeza maeneo salama na yenye faida.
Ninajua fedha wanazolipwa wastaafu zikitumika vizuri zinaweza kutoa
mchango mkubwa katika kuendeleza miradi mbalimbali ya kiuchumi, kutoa ajira na
pia kuongeza pato la mstaafu na taifa.” Alisema.
Mkurugenzi
wa Uwekezaji wa Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma PSSSF, Bw. Fortunatus
Magambo (kulia), akikabidhi mche wa Parachichi kwa mmoja wa wastaafu watarajiwa
wa Mfuko huo, Bw. Thadeo Daniel Deo, Afisa Mtendaji Mtaa
Mangaveta Jijini Mbeya kwenye semina ya maandalizi ya kustaafu utumishi wa umma
kwenye ukumnbi wa Mkapa jijini Mbeya leo Septemba 19, 2023. Katikati ni
Mkurugenzi wa Ununuzi na Ugavi, PSSSF, Bw. Ernest Khisombi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...