Na Mwandishi wetu, Mirerani

SHIRIKA lisilo la kiserikali la Haki Madini, limewajengea uwezo wanawake 21 wadau wa madini ya Tanzanite wakiwemo mabroka, waongeza thamani, wachekechaji, wauza magonga na wajasiriamali.

Ofisa miradi wa shirika la Haki Madini Emmanuel Mbise amesema mafunzo hayo ya siku 10 yatawajengea uwezo wanawake hao wa sekta ya madini ya Tanzanite na vito kwa ujumla ili waongeze pato lao.

Mbise amesema ni muda mrefu sasa wanaume wananufaika zaidi na sekta ya madini hivyo wamewajengea uwezo wanawake hao wanufaike nao kupitia kuongeza thamani ya madini ya Tanzanite na vito.


"Serikali imetenga eneo la mji mdogo wa Mirerani, liwe la kuongea thamani madini ya Tanzanite na vito, nasi tukaona tutumie fursa hiyo kwa kuwajengea uwezo wanawake ili nao wasiachwe nyuma washiriki kwa ujumla," amesema.


Ofisa madini mkazi (RMO) Mirerani Nchagwa Chacha Marwa akifungua mafunzo hayo amewataka wanawake hao kuyatumia ili wanufaike zaidi kwani wataongezewa uwezo.


RMO Marwa amewapongeza Haki Madini kwa kuandaa mafunzo hayo yatakayowanufaisha wanawake hao wa eneo hilo.


"Ni fursa kubwa na nzuri mmepata wanawake wadau wa madini kupitia shirika la Haki Madini hivyo tuyatumie ipasavyo kwa kuona mabadiko pindi mkihitimu, hongereni sana," amesema RMO Chacha.


Ofisa madini jinsia wa shirika Haki Madini, Joyce Ndakaru amesema mafunzo hayo yana kusudi kubwa la kuongeza ushiriki wa wanawake na unufaikaji kupitia madini ya Tanzanite na vito kwa ujumla.


Ndakaru amesema dhana ya kuwa sekta ya madini inahitaji nguvu pekee siyo sahihi kwani pia ina lenga wanawake kuhakikisha wanashiriki na kunufaika na madini ya Tanzanite kupitia kuyaongeza thamani.


Amesema maendeleo kwenye sekta hiyo yatapatikana endapo wanawake wakiingia kwenye kuongeza thamani wakitumia nguvu ya akili na siyo nguvu ya mwili pekee.


"Wanawake wakiwa waelewa wa sekta husika wataweza kuongeza thamani ya madini kwa manufaa yao wenyewe na jamii inayowazunguka kwa ujumla," amesema.


Mmoja kati ya washiriki wa mafunzo hayo Rachel Njau amewashukuru Haki Madini kwa kufanikisha mafunzo hayo kwa wanawake wadau wa madini ya Tanzanite.


Njau ambaye ni Katibu wa chama cha wachimbaji madini Mkoani Manyara (MAREMA) Tawi la Mirerani, amesema wanawake hao watayatumia mafunzo hayo kwa kunufaika zaidi tofauti na awali kabla ya kupata mafunzo hayo.



Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...