Na Mwandishi Wetu

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Moses Nnauye (Mb) amesema wizara imeendelea kuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha inawekeza na kukuza matumizi ya TEHAMA nchini.

Ameyasema hayo, leo Januari 26, 2024 wakati akishuhudia utiaji saini wa hati ya makubaliano ya ushirikiano kati ya Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Benki ya NMB uliofanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam.

"Hafla hii ya utiaji saini wa hati ya ushirikiano kati ya wizara na NMB inaweka historia na kuthibitisha kuwa, TEHAMA na mabadiliko ya kidigitali nchini ni masuala mtambuka yanayogusa Sekta ya Umma, Sekta Binafsi na wananchi kwa ujumla, amesema Mhe. Nape.

Mhe. Waziri Nape ameeleza kuwa utekelezaji wa ushirikiano huu unalenga Serikali na Sekta Binafsi inakuwa na mifumo bora na rafiki ya utoaji wa huduma kwa wananchi inayotumia teknolojia za kisasa, mazingira wezeshi ya kutumia TEHAMA nchini na kuhakikisha tunakuza vipaji vya vijana kwenye masuala ya TEHAMA.

Kwa upande mwingine ushirikiano huu unalenga kuongeza idadi ya vituo vya ubunifu katika maeneo mbalimbali ya nchini na eneo la ujumuishi wa kifedha wa kidigitali kwa kuongeza wigo wa utumiaji wa fedha kwa njia ya kidigitali.

Akitoa salamu za Benki ya NMB Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki hiyo Bi. Ruth Zaipuna amesema kuwa kwa muda mrefu Benki ya NMB imekuwa mshirika mkubwa wa Serikali katika kuchagiza Sera ya Uchumi wa Kidigitali, pamoja na kuunda na kuboresha mifumo mbalimbali ya TEHAMA.

Amesema kuwa Benki ya NMB imewekeza na kuwa Benki yenye Kituo cha Kutunza Taarifa (Data Center) ya kisasa, mifumo imara na ya kisasa ya TEHAMA, Teknolojia za kisasa za kulinda usalama wa mifumo na taarifa za Benki na za wateja wake na mifumo ya kisasa ya kusaidia ubunifu.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Bwana Mohammed Khamis Abdullah amesema wizara imeshirikiana na NMB katika masuala mbalimbali ikiwemo uandaaji wa Mkakati wa miaka 10 wa uchumi wa kidigitali, uandaaji wa Sera Mpya ya TEHAMA ya 2024 na ujenzi wa mfumo wa kuwatambua wateja (eKYC - electronic Know Your Customer).

"Tumeanza maandalizi ya kutayarisha Sheria ya TEHAMA nchini baada ya kukamilika kwa Sera ya TEHAMA 2024 ambayo ipo kwenye hatua za mwisho za uidhinishwaji",alisema Katibu Mkuu huyo.

Hafla ya utiaji saini wa hati ya makubaliano ya ushirikiano kati ya Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na Benki ya NMB imewakutanisha maafisa waandamizi wa wizara na wataalam wa TEHAMA waliiongozwa na Bw. Mohamed Mashaka ambaye ni Mkurugenzi wa Uendelezaji wa Mifumo na Huduma za TEHAMA na kwa NMB waliongozwa na Bw. Kwame Makundi, Afisa Mkuu wa Teknolojia na Mabadiliko ya Kidigitali wa Benki ya NMB.









Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...