NA K-VIS BLOG/KHALFAN SAID, SONGEA

SERIKALI imewahakikishia Waheshimiwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, kuwa inayachukulia kwa uzito mkubwa, maoni na mapendekezo yao kuhusu maboresho ya Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi

Kauli hiyo ya Serikali imetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Joyce Ndalichako, wakati akifunga Kikao Kazi cha Mafunzo ya Uelimishaji kwa Waheshimiwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Kanda ya Kusini na Watendaji wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) mjini Songea, Februari 10, 2024.

Akieleza zaidi Mhe. Profesa Ndalichako amesema tayari inayafanyia kazi baadhi ya mapendekezo ya maboresho ya sheria yaliyotolewa na waheshimiwa Majaji kwenye kikao kazi kama hicho kilichofanyika mjini Bagamoyo mwezi Julai, 2023

“Mapendekezo ya kuboresha kifungu cha 39 (2) cha Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi [Sura 263] kilichoweka ukomo wa muda wa kuwasilisha madai bila kutoa wigo wa kupokea madai hayo iwapo kuna sababu za msingi za kucheleshwa, tumeyafanyia kazi na tunataraji muswada wa marekebisho kuwasilishwa bungeni hivi karibuni.” Amesema Mhe. Profesa Ndalichako.

Aidha, Mhe. Profesa Ndalichako amesema Ofisi yake kupitia Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi inatarajia kupokea maoni zaidi kutoka kwa waheshimiwa majaji kwa lengo la kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi [Sura 263].

“Natamani kuona kuwa kati ya mapendekezo yenu katika mafunzo haya iwe ni namna gani rahisi tunaweza kutumia sheria kuwezesha waajiri wote ambao hawajajisajili WCF, kufanya hivyo mara moja,” amesema

Mhe. Profesa Ndalichako pia amebainisha kuwa Serikali ya awamu ya Sita chini ya Uongozi mahiri wa Mheshimiwa Daktari Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatambua na kuthamini mchango wa wafanyakazi katika sekta zote na ndio maana imeendelea kutekeleza na kuboresha masuala ya fidia kwa wafanyakazi katika sekta binafsi na umma

Amesema, katika kipindi kifupi cha Uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita kumeshuhudiwa mabadiliko mbalimbali katika sekta ya hifadhi ya jamii ikiwemo kupunguza kiwango cha uchangiaji kwa waajiri wa sekta binafsi kutoka asilimia 1 ya mshahara wa mfanyakazi kila mwezi hadi kufikia asilimia 0.5;

Awali akifungua mafunzo hayo mwishoni mwa juma, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani aliwahimiza waajiri nchini kujisajili WCF na kutoa taarifa za ajira za wafanyakazi wao ili kulinda haki za wafanyakazi hao pindi wanapopatwa na majanga wakiwa kazini.

"Pamoja na uwepo wa sheria inayowabana waajiri wanaoshindwa kuwasajili wafanyakazi wao WCF lakini bado kuna waajiri ambao hawatoi taarifa za ajira za wafanyakazi wao na hivyo kuuweka mfuko katika nafasi ngumu ya kutekeleza majukumu yake," alifafanua

Jaji Siyani ametoa mfano wa kisa cha mfanyakazi mmoja aliyekuwa akifanya kazi kwenye kampuni moja ya ujenzi mkoani Lindi ambaye aliumia akiwa kazini na kupelekea kupoteza  baadhi ya viungo vyake na kumsababishia ulemavu wa kudumu kwa zaidi ya asilimia 75 lakini alikosa vigezo vya kupata fidia kwa kuwa mwajiri wake hakuwa amejisajili na kuwasilisha michango WCF kwa mujibu wa sheria.

“Licha ya kijana huyo kufanya kazi kwa zaidi ya miaka miwili lakini taarifa zake hazikuwepo WCF na hivyo kukosa haki ya kupata fidia yoyote” ameeleza Jaji Siyani; na kuongeza kuwa iwapo zingekuwepo taarifa za mfanyakazi huyo, bila shaka angepata fidia bora zaidi ya ile iliyotokana na majadiliano na maridhiano na mwajiri wake.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Dkt. John Mduma, amesema Mahakama ya Tanzania ni wadau muhimu wa Mfuko huo katika utekelezaji wa majukumu yake kwa kuwa Mfuko unategemea maamuzi mbalimbali ya mahakama katika utekelezaji wake wa majukumu ikiwemo maamuzi ya kesi za mirathi.

Dkt. Mduma amesema kuwa mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Serikali  yanayozitaka  taasisi zake kuhakikisha zinashirikiana kwa karibu kwa dhumuni la kuongeza tija na huduma bora kwa wananchi.

Pia, mafunzo hayo yanatoa fursa ya kubadilishana uzoefu baina ya wataalam wa Mahakama na WCF kupitia mada mbalimbali zitakazowasilishwa ambapo washiriki wanaweza kuja na mapendekezo yatakayoboresha utendaji kazi wa Mfuko huo.

"Ni matarajio yangu kuwa mafunzo haya yataleta manufaa makubwa kwa pande zote mbili, ikiwemo kuimarisha mahusiano kwa lengo la kutoa huduma bora kwa wananchi na kuchangia kukuza uchumi wa nchi yetu na hasa kupunguza umasikini kwa wafanyakazi watakaopata majanga yanayotokana na kazi zao," amesisitiza Dkt. Mduma.

Mafunzo hayo ambayo ni ya awamu ya nne yamewaleta pamoja washiriki kutoka mikoa ya Ruvuma, Mtwara, Iringa, Mbeya, Songwe na Rukwa ambapo miongoni mwa mada zinazotarajiwa kuwasilishwa ni kuhusu sheria ya fidia kwa wafanyakazi, taratibu za uwasilishaji na ushughulikiaji wa madai ya fidia kwa wafanyakazi.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Joyce Ndalichako, akizungumza wakati akifunga Kikao kazi cha Mafunzo ya Uelimishaji kwa Waheshimiwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania - Divisheni ya Kazi, Kanda ya Kusini, iliyofanyika Februari 10, 2024.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Joyce Ndalichako (katikati) akizungumza wakati akifunga Kikao kazi cha Mafunzo ya Uelimishaji kwa Waheshimiwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania - Divisheni ya Kazi, Kanda ya Kusini, iliyofanyika Februari 10, 2024. Wengine pichani ni Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma (kushoto) na kulia ni Mhe. Joseph Karayemaha, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Songea.

Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma, akizungumza kwenye kikao kazi cha Mafunzo ya Uelimishaji kwa Waheshimiwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania - Divisheni ya Kazi, Kanda ya Kusini, kilichofanyika mjini Songea, Februari 10, 2024.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu-Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina,  akizungumza kwenye kikao kazi cha Mafunzo ya Uelimishaji kwa Waheshimiwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania - Divisheni ya Kazi, Kanda ya Kusini, kilichofanyika mjini Songea, Februari 10, 2024.
Baadhi ya Washiriki wakimsikiliza Mhe. Waziri.
Baadhi ya Washiriki wakimsikiliza Mhe. Waziri.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu-Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (kushoto) akipongezana na Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma huku Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Songea, Mhe. Joseph Karayemaha, akishuhudia mwishoni mwa kikao kazi hicho.






Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...