Na mwandishi wetu

Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) ya jijini Dodoma inatarajia kuanzisha ushirikiano wa matibabu na Hospitali ya Rufaa ya Mjini Magharibi (Lumumba), Zanzibar katika huduma za kibingwa.

Ushirikiano huu utalenga kubadilishana uzoefu kati ya Hospitali hizi mbili za umma.

Akiongea, Naibu Waziri wa Afya Zanzibar Mhe.Hassan Khamis Hafidh, amepongeza ujio wa Viongozi wa BMH na kuwa Hospitali ya Lumumba itanufaika kwa kubadilishana uzoefu.

"Nimefika Hospitali ya Benjamin Mkapa Dodoma nikajionea utayari wa Madaktari Bingwa na Vifaa vya kisasa mnavyovitumia, nimefika kwenye wodi maalumu ya Uloto nikiri kwamba naona fahari kuja kwenu hapa maana yapo mengi tutakayo chukua kupitia ushirikiano huu," amesema Mhe Naibu Waziri.

Ameyasema hayo wakati uongozi wa Hospitali ya Benjamin Mkapa ulipomtembelea ofisini kwake.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu Bi. Prisca Lwangili, akimwakilisha Mkurugenzi Mtendaji wa BMH, amesema "Hospitali ya Benjamin Mkapa imekuwa kwa kasi na kutoa matibabu ambayo hayapatikani Afrika Mashariki na Kati.

"Hivyo tumeona ni muhimu kusogeza huduma hizi hapa Zanzibar kwa kuwa hapa pia kuna uhitaji wa huduma za Upandikizaji Uloto ili kutibu seli mundu," amesema.

Kwa mujibu wa Kaimu Mkurugenzi wa Utafiti na Mafunzo wa BMH, Bi. Monica Kessy, uhusiano huu ni sehemu ya wajibu wa BMH ili kubadilishana uzoefu kati ya hospitali za umma.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Upasuaji BMH, Dkt. Januarius Hinju, ameeleza utayari kwa Madaktari Bingwa wa BMH katika huduma.

"Madaktari Bingwa wa BMH tupo tayari kushirikiana na wenzetu ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora," ameongeza.




Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...