MAHAKAMA ya Rufani leo imeshindwa kuendelea na usikilizwaji wa shauri la rufaa lililokatwa na Benki ya Equity Bank Tanzania Limited na Equity Bank Kenya Limited dhidi ya kampuni ya mafuta ya State Oil, kutokana na kesi ya msingi kusikilizwa bila hati ya madai kufanyiwa marekebisho.

Benki zilikata rufaa hiyo kupinga hukumu ya Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara iliyoipa ushindi kampuni ya State Oil inayodaiwa kukataa kulipa mkopo iliyopewa na benki hizo wa USD 18,640,000.

Rufaa hiyo ilikuwa imepangwa kusikilizwa leo tarehe 23, 2024 mbele ya jopo la majaji Rehema Mkuye, Abraham Mwampash na Zainabu Muruke.

Lakini majaji hao kabla ya kuanza kusikiliza rufaa hiyo wakawahoji mawakili kama ni sawa kesi ya msingi kusikilizwa bila hati ya madai kufanyiwa marekebisho baada ya Equity benki ya Kenya kujiunga katika kesi hiyo.

Mawakili wanaoziwakilisha benki hizo, Mpaya Kamala na Timon Vitalis wameieleza mahakama kuwa japo kweli kanuni zinasema kuwa baada ya kuongezwa mdaiwa mwingine hati ya madai ilipaswa kufanyiwa marekebisho, lakini wao hawaoni kama kutokufanya marekebisho ni tatizo kwani kutokufanya hivyo hakukuathiri upande wowote.

Mawakili hao kwa nyakati tofauti wamesema kuwa hata hivyo amri ya 1, Kanuni ya 10 (4) za Mwenendo wa Mashauri ya Madai (CPC) inampa jaji uhuru wa kuamua vinginevyo badala ya kuamuru hati ya madai kufanyiwa marekebisho na kwamba ndivyo jaji aliyesikiliza kesi hiyo ya msingi alivyoamuru.

“Hapa baada ya mdaiwa wa pili, Equity Kenya kuunganishwa jaji aliamuru kuwa wadaiwa wawasilishe maelezo yao ya utetezi wa maandishi. Na sisi tunaona hakukuwa na tatizo kwani hakukuathiri upande wowote”, amesema wakili Kamara.

Wakili wa kampuni ya State Oili Frank Mwalongo naye amesema kuwa anakubaliana na hoja za mawakili wenzake kuwa haikuwa muhimu kufanya marekebisho ya hati ya madai kwa kuwa kutokufanya hivyo hakujaathiri upande wowote.

“Kwa hiyo naiomba mahakama ione kwamba hoja hii haikuathiri upande wowote na Jaji alitenda kwa mujibu wa sheria na tuendelee na usikilizwaji wa rufaa.”

Baada ya mawakili hao kumaliza kutoa hoja zao kuhusu suala hilo, Jaji Mkuye ameahirisha kesi hiyo akisema kuwa mahakama itawajulisha pande zote siku ya kutoa uamuzi utakapokuwa tayari.

Kampuni ya State Oil inadaiwa kuwa ilidhaminiwa na Benki ya Equity Kenya kuchukua mkopo wa USD 18,640,000 kutoka kwa kampuni Lamar Commodity Trading DMMC ya Dubai, huku na yenyewe ikiikabidhi Benki ya Equity ya Kenya hati za mali zake mbalimbali kama dhamana ya udhamini wa mkopo huo.

Indaiwa kuwa hata hivyo haikuweza kulipa mkopo huo, hivyo Benki ya Equity Tanzania kama mdhamini wake ndio ikalipa mkopo huo kwa kampuni ya Lamar Commodity.

Benki ya Equity Kenya baada ya kuanza kuidai kampuni hiyo mkopo huo kupitia kwa Benki ya Equity Tanzania, ambayo ndio iliyopewa jukumu la kusimamia dhamana zilizowekwa na State Oil, kampuni hiyo ilikimbilia mahakamani ambako iliifungulia kesi Benki ya Equity Tanzania ikipinga kudaiwa mkopo huo.

Kabla ya kesi hiyo kuanza kusikilizwa Benki ya Equity Tanzania iliwasilisha maombi mahakamani hapo ili Benki ya Equity Kenya nayo ijumuishwe kwenye kesi hiyo na Jaji aliyeisikiliza akaikubalia akaamuru Benki ya Equity Kenya nayo ikaunganishwa kwenye kesi hiyo.

Benki hiyo ya Kenya ilipounganishwa mahakama haikutoa amri ya kufanya marekebishoa ya hati ya madai badala yake iliamuru tu benki hizo ambazo zilikuwa wadaiwa katika kesi hiyo ziwasilishe utetezi wake wa maandishi, kisha ikaendelea na usikilizwaji mpaka ikatoa hukumu.

Katika kesi hiyo kampuni hiyo iliiomba mahakama itamke kuwa ilishalipa mkopo wake wote iliokuwa inadaiwa na kwamba haina benki hizo hazina madai yoyote dhidi yake na pia ikaomba mahakama iamuru irejeshewe hati za mali zake ilizokuwa imezitoa kama dhamana ya kupata udhamini wa mkopo huo.

Benki katika utetezi wake ziliita mashahidi sita akiwemo na mwakilishi wa kampuni ya Lamar aliyetoa ushahidi jinsi alivyoikopesha State Oil fedha hizo kwa kudhaminiwa na Benki ya Equity na kwamba ilishindwa kurejesha mkopo huo na ikabidi benki hiyo iliyomdhamini ndio ikalipa mkopo huo.

Mahakama hiyo katika hukumu yake iliyotolewa Oktoba Mosi, 2021, ilikubaliana na madai na ushahidi wa State Oil kupitia kwa shahidi wake mmoja, kuwa ilikuwa imeshalipa deni lake lote na hivyo benki hizo hazikuwa na madai dhidi yake na ikaamuru State Oil irejeshewe hati zake za mali ilizoweka dhamana.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...