Balozi wa Pakistani nchini Siraj Ahmad Khan (kushoto), Mkurugenzi wa Biashara wa Vodacom Tanzania, Linda Riwa (katikati) na Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya Digit, Abdul Rehman Mahmood (kulia) wakiwa kwenye picha ya pamoja wakati wa uzinduzi wa simu maalum iitwayo Smart Kitochi+ kwa ajili ya watu wenye ulemavu wa kuona na kusikia huku ikiongeza matumizi ya dijitali nchini, hafla hiyo ilifanyika jana jijini Dar es Salaam.





Ili kuimarisha ushirikishwaji na kuongeza matumizi ya huduma na bidhaa za kidijitali nchini, kampuni ya teknolojia na mawasiliano ya Vodacom Tanzania PLC imezindua simujanja ya kidijitali inayoitwa 'Smart Kitochi +' ambayo imeundwa ikiwa na vipengele muhimu kwa ajili ya wateja wasiosikia na wasioona.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi jijini Dar es Salaam leo, Mkurugenzi wa Biashara wa kampuni hiyo, Bi. Linda Riwa, amesema kuwa uzinduzi huu ni sehemu ya juhudi endelevu za kampuni hiyo za kukuza ushirikishwaji huku ikiunga mkono serikali katika azma yake ya kuchochea matumizi ya bidhaa na huduma za kidigitali.

"Tunafurahia mapinduzi haya ya kuleta bidhaa na huduma za kidigitali na za kibunifu kwa wateja wetu wenye mahitaji mbalimbali kote nchini. Leo, tunazindua simu ya kipekee ya kidijitali inayoitwa 'Smart Kitochi+' ambayo mbali na sifa kama kioo kikubwa na cha kugusa, uwezo mkubwa wa kuhifadhi na betri inayodumu muda mrefu, simu hii pia itawanufaisha wateja wetu wenye ulemavu wa kusikia na kuona,” anasema Linda.

“Simu hii inajumuisha teknolojia ya kugusa na sauti, ikiruhusu wateja wenye changamoto hizi kupata huduma zetu bila kutegemea msaada wa mtu mwingine. Haya ni mapinduzi muhimu katika sekta ya utoaji huduma za mawasiliano, ikizingatiwa kuwa serikali inahimiza watoa huduma kuzingatia ushirikishwaji katika utoaji wa huduma kwa wateja,” aliongeza Linda.

Uzinduzi wa simu hii ni ingizo la kipekee sokoni ukilinganisha na matoleo mengine, ikiwa na uwezo wa kuchochea ushirikishwaji katika matumizi ya huduma za mawasiliano ya kidigitali. Pia ina ubora wa hali ya juu ikiwa na kioo kikubwa na cha kugusa (2.8”), uwezo mkubwa wa kuhifadhi vitu kwenye 8GB na betri inayodumu muda mrefu ya 3000mAh.

Toleo hili jipya la 'Smart Kitochi+' ni sehemu ya juhudi za Vodacom kuwapeleka wateja wake kwenye matumizi ya kidigitali, ikiwa ni pamoja na mtandao wa 4G, ambao bado una watumiaji wachache ikilinganishwa na idadi ya watumiaji wa simu za mkononi nchini Tanzania.

"Tunajivunia kuwa mtandao unaoongoza nchini, tukitoa huduma za kidigitali za ubunifu kwa zaidi ya wateja milioni 21. Kuwa na idadi kubwa ya wateja pekee haitoshi; tunataka wateja wetu wanufaike na mapinduzi ya kidigitali yanayoendelea na ubunifu mkubwa tunaoingiza kwenye bidhaa zetu. Kwa kuanzisha bidhaa za kisasa kama 'Smart Kitochi+' tunaamini tutachochea wateja wengi zaidi kuhama kutoka kwenye mfumo wa 2G na kuanza kufurahia huduma mbalimbali za kidigitali zinazotolewa na mtandao wetu wa kasi wa 4G na 5G uliosambaa nchini na hatimaye kuongeza matumizi ya simujanja ambayo kwa sasa ni asilimia 32," alifafanua Bi. Linda.

Akizungumzia simu hiyo mpya, Mwenyekiti wa Chama cha Viziwi Tanzania (TLB) Bw. Luis Benedicto aliisifia simu hiyo akikiri kuwa itakuwa mkombozi kwa watu wenye ulemavu wa kusikia na kuona.

"Tulikuwa tumetengwa na kubanwa katika matumizi ya simu za mkononi, kwani nyingi hazikuwa rafiki kwa watu wenye ulemavu wa kusikia na kuona. Kuzinduliwa kwa simu hii kutatusaidia sio tu kufurahia huduma za mawasiliano kutoka Vodacom bali pia kuimarisha mwingiliano wetu na wengine na kutumia simu hizi kwa manufaa ya kijamii na kiuchumi," alielezea Bw. Benedicto.

Uzinduzi huu unakuja baada ya hivi karibuni kampuni hiyo kuanzisha dawati maalum kwa ajili ya kuhudumia wateja wasioona baada ya kuanzisha dawati kama hilo kwa ajili ya wateja wenye ulemavu wa kusikia mwaka jana.

Juhudi za kampuni hiyo katika kuzingatia na kuboresha maisha ya wateja wake ili kupunguza au kufuta kabisa utofauti uliopo wa kidigitali kwa watu wenye ulemavu zimeifanya iwe miongoni mwa watia saini wa miongozo ya GSMA kwa kuchochea ushirikishwaji wa kidigitali kwa watu wenye ulemavu. Miongozo hiyo huweka misingi ya hatua za kuchukua pamoja na kinachotakiwa kufanywa na mtoa huduma za simu za mkononi ili kupunguza pengo katika upatikanaji wa huduma pamoja na matumizi ya huduma hizo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...