Dar es Salaam, 11 Mei 2024

Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) inaujulisha umma kuwa taarifa inayosambaa kuhusu ndege yake aina ya Boeing 787- 8 yenye usajili wa namba 5H-TCJ kupelekwa kwenye matengenezo makubwa yaani Check - C kabla ya kufikisha muda wake tangu inunuliwe na kutelekezwa nchini Malaysia sio za kweli.

Ndege yake ya B787- 8 ipo nchini Malaysia kwa ajili ya matengenezo ya lazima ya injini zake baada ya kufikisha muda wake na sio matengenezo makubwa ya Check - C.

“Matengenezo makubwa ya ndege zetu za 787 – 8 (Dreamliner) yanafanyika hapa nchini kwenye Karakana yetu ya KIMAFA iliyopo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro kila baada ya miaka 3 au masaa 12,000 chochote kitakachoanza. Karakana zetu zina wataalam wenye uzoefu wa kufanya matengenezo makubwa ya ndege ya kiwango cha Check – C”, amesema Mha. Matindi.

Ameongeza kuwa tangu ndege hizi ziwasili nchini zimefanyiwa matengenezo makubwa (Check - C) mara moja ambapo kwa ndege ya kwanza iliyowasili nchini mwaka 2018 ilifanyiwa matengenezo hayo mwaka 2021 na ya pili iliyowasili mwaka 2019 ilifanyiwa matengenezo mwaka 2022, amehitimisha, Mha. Matindi.

Tatizo la ndege kukaa muda mrefu kwenye karakana, Malaysia, linatokana na uhaba wa injini za ziada ambazo zingeweza kutumika wakati injini zake zikifanyiwa matengenezo.

Ndege za Boeing 787- 8 za ATCL zinatumia injini za Kampuni ya Rolls Royce aina ya Trent 1000. Kwa mujibu wa miongozo ya Mamlaka za Usafiri wa Anga na watengenezaji wa injini hizo, imekuwa ni lazima injini hizo kufanyiwa matengenezo makubwa (overhaul) kila baada ya miruko 1,000. Hii ni baada ya kugundulika kwa matatizo ya kisanifu (design) katika mifumo hasa ya ufuaji wa nguvu za kuendesha ndege, kwa injini nyingi za matoleo mapya. Aidha, Matatizo haya yamesababisha kutolewa kwa miongozo maalum kuhusu uchunguzi wa injini wa mara kwa mara iwapo katika matumizi.

Injini hizo zinapopelekwa kwa matengenezo zinalazimika kuzingatia foleni au zamu (slot) kutokana na idadi kubwa ya injini zinazosubiria matengenezo na hivyo kupelekea kuchukua muda mrefu kuhitimisha matengenezo yake. Kukosekana kwa injini za ziada kunasababisha ndege isubiri hapo karakana hadi kukamilika kwa matengenezo tajwa.

Kwa sasa matengenezo ya injini za ndege yetu iliyoko Malaysia tayari yanaendelea na inatarajiwa kurejea nchini mwanzoni mwa mwezi Juni 2024.

Imetolewa na:

Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...